કુરઆન મજીદના શબ્દોનું ભાષાંતર - સવાહિલી ભાષાતર - અબ્દુલ્લાહ મુહમ્મદ અને નાસિર ખમીસ * - ભાષાંતરોની અનુક્રમણિકા


શબ્દોનું ભાષાંતર સૂરહ: અશ્ શુઅરાઅ   આયત:

Surat Ash-Shu'ara

طسٓمٓ
«Ṭā, Sīn, Mīm.» Yametangulia maelezo kuhusu herufi za mkato mwanzo wa sura ya Al-Baqarah.
અરબી તફસીરો:
تِلۡكَ ءَايَٰتُ ٱلۡكِتَٰبِ ٱلۡمُبِينِ
Hizi ni aya za Qur’ani yenye kufafanua kila kitu, yenye kupambanua baina ya uongofu na upotevu.
અરબી તફસીરો:
لَعَلَّكَ بَٰخِعٞ نَّفۡسَكَ أَلَّا يَكُونُواْ مُؤۡمِنِينَ
Huenda wewe, ewe Mtume, kwa kuwa una hamu sana ya kutaka wao waongoke, ukajiangamiza mwenyewe kwa kuwa wao hawakukuamini na hawakufuata kimatendo uongofu wako. Basi usifanye hivyo.
અરબી તફસીરો:
إِن نَّشَأۡ نُنَزِّلۡ عَلَيۡهِم مِّنَ ٱلسَّمَآءِ ءَايَةٗ فَظَلَّتۡ أَعۡنَٰقُهُمۡ لَهَا خَٰضِعِينَ
Tukitaka tutawateremshia wakanushaji, miongoni mwa watu wako, miujiza itokayo mbinguni yenye kuwaogopesha itakayowalazimisha wao kuamini, na hapo shingo zao ziwe zimenyongeka na kudhalilika. Lakini hatukutaka hilo, kwani Imani yenye kunufaisha ni kuyaamini yaliyoghibu kwa hiyari.[8]
[8]Rudia sura ya Al-Baqarah aya:3, kwa maelezo zaidi kuhusu ghayb (Yaliyoghibu)
અરબી તફસીરો:
وَمَا يَأۡتِيهِم مِّن ذِكۡرٖ مِّنَ ٱلرَّحۡمَٰنِ مُحۡدَثٍ إِلَّا كَانُواْ عَنۡهُ مُعۡرِضِينَ
Na hauwajii washirikina hawa ukumbusho, kutoka kwa Mwingi wa rehema unaoanzwa kuteremshwa, kitu baada ya kitu, wenye kuwaamrisha na kuwakataza na kuwakumbusha Dini ya kweli, isipokuwa wanaupa mgongo na hawaukubali.
અરબી તફસીરો:
فَقَدۡ كَذَّبُواْ فَسَيَأۡتِيهِمۡ أَنۢبَٰٓؤُاْ مَا كَانُواْ بِهِۦ يَسۡتَهۡزِءُونَ
Kwa hakika washaikanusha Qur’ani na washaifanyia shere, basi zitawajia wao habari za jambo ambalo walikuwa wakilifanyia shere na dharau, na itawashukia wao adhabu ikiwa ni malipo ya kumuasi Mola wao.
અરબી તફસીરો:
أَوَلَمۡ يَرَوۡاْ إِلَى ٱلۡأَرۡضِ كَمۡ أَنۢبَتۡنَا فِيهَا مِن كُلِّ زَوۡجٖ كَرِيمٍ
Je, wanakanusha na hali wao hawakuiangalia ardhi ambayo ndani yake tumeotesha kila aina nzuri ya mimea ambayo hakuna awezae kuiyotesha isipokuwa Mola wa viumbe vyote?
અરબી તફસીરો:
إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَأٓيَةٗۖ وَمَا كَانَ أَكۡثَرُهُم مُّؤۡمِنِينَ
Kwa hakika, katika kuitoa mimea kwenye ardhi ni dalili wazi ya ukamilifu wa uweza wa Mwenyezi Mungu, na wengi wa watu hawakuwa ni wenye kuamini.
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ ٱلۡعَزِيزُ ٱلرَّحِيمُ
Na kwa hakika Mola wako Ndiye Mshindi wa kila kiumbe, ni Mwenye kurehemu Ambaye rehema Yake imeenea kila kitu.
અરબી તફસીરો:
وَإِذۡ نَادَىٰ رَبُّكَ مُوسَىٰٓ أَنِ ٱئۡتِ ٱلۡقَوۡمَ ٱلظَّٰلِمِينَ
Na wakumbushe watu wako, ewe Mtume, pindi Mola wako Alipomuita Mūsā kuwa awaendee watu madhalimu,
અરબી તફસીરો:
قَوۡمَ فِرۡعَوۡنَۚ أَلَا يَتَّقُونَ
nao ni watu wa Fir’awn na uwaambie wayaogope mateso ya Mwenyezi Mungu Aliyetukuka na waache ukafiri na upotevu walionao.
અરબી તફસીરો:
قَالَ رَبِّ إِنِّيٓ أَخَافُ أَن يُكَذِّبُونِ
Mūsā akasema, «Mola wangu! Mimi ninaogopa wasije wakanikanusha juu ya utume,
અરબી તફસીરો:
وَيَضِيقُ صَدۡرِي وَلَا يَنطَلِقُ لِسَانِي فَأَرۡسِلۡ إِلَىٰ هَٰرُونَ
na moyo wangu ukaingia kero kwa kunikanusha, na ulimi wangu usiwe na ufasaha wa kulingania. Basi mtume Jibrili aende na wahyi kwa ndugu yangu Hārūn, ili anisaidie na aniamini kwa ninayoyasema, na awafafanulie kile ninachowaambia, kwani yeye ana ufasaha zaidi wa matamshi kuliko mimi.
અરબી તફસીરો:
وَلَهُمۡ عَلَيَّ ذَنۢبٞ فَأَخَافُ أَن يَقۡتُلُونِ
Na watanishika na kosa la kumuua mwanamume wa jamii ya Qibṭī miongoni mwao, na kwa hivyo ninaogopa wasiniue kwa ajili yake.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ كَلَّاۖ فَٱذۡهَبَا بِـَٔايَٰتِنَآۖ إِنَّا مَعَكُم مُّسۡتَمِعُونَ
Mwenyezi Mungu Akamwambia Mūsā, «Sivyo hivyo! Hawatakuua. Na nimekubali matakwa yako juu ya Hārūn. Basi endeni mkiwa na miujiza yenye kuonyesha ukweli wenu. Sisi tuko pamoja na nyinyi kwa ujuzi, utunzi na usaidizi tunasikiliza.
અરબી તફસીરો:
فَأۡتِيَا فِرۡعَوۡنَ فَقُولَآ إِنَّا رَسُولُ رَبِّ ٱلۡعَٰلَمِينَ
Mjieni Fir’awn na mumwambie, «Sisi tumetumwa kwako na kwa watu wako kutoka kwa Mola wa viumbe wote
અરબી તફસીરો:
أَنۡ أَرۡسِلۡ مَعَنَا بَنِيٓ إِسۡرَٰٓءِيلَ
kwamba uwaache Wana wa Isrāīl waende na sisi.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ أَلَمۡ نُرَبِّكَ فِينَا وَلِيدٗا وَلَبِثۡتَ فِينَا مِنۡ عُمُرِكَ سِنِينَ
Fir’awn akasema kumwambia Mūsā kwa kumsimanga, «Je, hatukukulea kwenye majumba yetu ukiwa mchanga, ukakaa kwenye utunzi wetu miaka (mingi) katika umri wako,
અરબી તફસીરો:
وَفَعَلۡتَ فَعۡلَتَكَ ٱلَّتِي فَعَلۡتَ وَأَنتَ مِنَ ٱلۡكَٰفِرِينَ
ukafanya tendo la jinai kwa kumuua mwanamume miongoni mwa watu wangu, ulipompiga na ukamsukuma, na wewe ni miongoni mwa wakanushaji neema zangu na kukataa uola wangu?
અરબી તફસીરો:
قَالَ فَعَلۡتُهَآ إِذٗا وَأَنَا۠ مِنَ ٱلضَّآلِّينَ
Mūsā akasema kumjibu Fir’awn, «Nilifanya uliyoyataja kabla Mwenyezi Mungu Hajaniletea wahyi na kunitumiliza kama Mtume,
અરબી તફસીરો:
فَفَرَرۡتُ مِنكُمۡ لَمَّا خِفۡتُكُمۡ فَوَهَبَ لِي رَبِّي حُكۡمٗا وَجَعَلَنِي مِنَ ٱلۡمُرۡسَلِينَ
ndipo nilitoka kwenu kwa kukimbia kuelekea Madyan nilipoogopa usije ukaniua kwa nililolifanya bila kukusudia, Na Mola wangu Akanitunuku unabii na elimu na Akanifanya ni miongoni mwa Mitume.
અરબી તફસીરો:
وَتِلۡكَ نِعۡمَةٞ تَمُنُّهَا عَلَيَّ أَنۡ عَبَّدتَّ بَنِيٓ إِسۡرَٰٓءِيلَ
Na kwani huko kulelewa nyumbani kwako unakuona ni neema kutoka kwako juu yangu, na hali wewe umewafanya Wana wa Isrāīl ni watumwa , unawachinja wana wao wa kiume na unawaachilia wanawake wao ili watumwe na wadharauliwe?»
અરબી તફસીરો:
قَالَ فِرۡعَوۡنُ وَمَا رَبُّ ٱلۡعَٰلَمِينَ
Fir’awn akamwambia Mūsā, «Na huyo Mola wa viumbe wote Ambaye unadai kwamba wewe ni mjumbe Wake, ni kitu gani?»
અરબી તફસીરો:
قَالَ رَبُّ ٱلسَّمَٰوَٰتِ وَٱلۡأَرۡضِ وَمَا بَيۡنَهُمَآۖ إِن كُنتُم مُّوقِنِينَ
Mūsā akasema, «Yeye ni Mmiliki na Mwenye kuipelekesha mbingu na ardhi na vilivyoko baina ya viwili hivyo. Iwapo nyinyi mna yakini na hilo, basi aminini.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ لِمَنۡ حَوۡلَهُۥٓ أَلَا تَسۡتَمِعُونَ
Fir’awn akasema kuwaambia walioko pambizoni mwake miongoni mwa watukufu wa watu wake, «Je, hamusikii maneno ya Mūsā ya ajabu kwamba kuna mola asiyekuwa mimi?»
અરબી તફસીરો:
قَالَ رَبُّكُمۡ وَرَبُّ ءَابَآئِكُمُ ٱلۡأَوَّلِينَ
Mūsā akasema, «Mola Ambaye mimi nawalingania nyinyi Kwake ni Yule Aliyewaumba nyinyi na Aliyewaumba wa mwanzo. Basi vipi nyinyi mnamuabudu ambaye ni kiumbe kama nyinyi na yeye ana mababa waliotoeka kama mababa zenu?»
અરબી તફસીરો:
قَالَ إِنَّ رَسُولَكُمُ ٱلَّذِيٓ أُرۡسِلَ إِلَيۡكُمۡ لَمَجۡنُونٞ
Fir’awn akasema kuwaambia wale watu wake makhsusi akiwapandisha ghadhabu zao, kwa kuwa Mūsā amemkanusha yeye, «Kwa kweli, huyu mjumbe wenu aliyeletwa kwenu ni mwendawazimu , asema maneno yasiyofahamika.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ رَبُّ ٱلۡمَشۡرِقِ وَٱلۡمَغۡرِبِ وَمَا بَيۡنَهُمَآۖ إِن كُنتُمۡ تَعۡقِلُونَ
Mūsā akasema, «Mola wa Mashariki na Magharibi na vilivyoko baina ya viwili hivyo, na vilivyomo ndani yake vya mwangaza na giza. Hili linapelekea kuwa ni lazima kumuamini Yeye Peke Yake, iwapo nyinyi ni miongoni mwa watu wa akili na kuzingatia.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ لَئِنِ ٱتَّخَذۡتَ إِلَٰهًا غَيۡرِي لَأَجۡعَلَنَّكَ مِنَ ٱلۡمَسۡجُونِينَ
Fir’awn akamwambia Mūsā kwa kumtisha, «Ukichukua mwingine aseyekuwa mimi ukamfanya ni mola nitakufunga jela pamoja na wale niliowafunga.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ أَوَلَوۡ جِئۡتُكَ بِشَيۡءٖ مُّبِينٖ
Mūsā akasema, «Je, utanifanya mimi ni miongoni mwa wafungwa jela, hata nikikuletea hoja ya kukata ambayo kwa hiyo utabainika ukweli wangu?»
અરબી તફસીરો:
قَالَ فَأۡتِ بِهِۦٓ إِن كُنتَ مِنَ ٱلصَّٰدِقِينَ
Fir’awn akasema, «Basi ilete ikiwa wewe ni miongoni mwa wakweli katika madai yako.»
અરબી તફસીરો:
فَأَلۡقَىٰ عَصَاهُ فَإِذَا هِيَ ثُعۡبَانٞ مُّبِينٞ
Hapo Mūsā akaitupa fimbo yake na ikageuka kuwa nyoka wa kikweli, si kiinimacho kama wanavyofanya wachawi.
અરબી તફસીરો:
وَنَزَعَ يَدَهُۥ فَإِذَا هِيَ بَيۡضَآءُ لِلنَّٰظِرِينَ
Na akautoa mkono wake kwenye uwazi wa kanzu yake uliofunguliwa kifuani au chini ya kwapa lake, na papo hapo ukawa mweupe kama barafu, na sio weupe wa mbalanga, ukawashangaza waangaliaji.
અરબી તફસીરો:
قَالَ لِلۡمَلَإِ حَوۡلَهُۥٓ إِنَّ هَٰذَا لَسَٰحِرٌ عَلِيمٞ
Fir’awn akasema kuwaambia watukufu wa watu wake, kwa kuogopa wasije wakaamini, «Kwa kweli Mūsā ni mchawi hodari.
અરબી તફસીરો:
يُرِيدُ أَن يُخۡرِجَكُم مِّنۡ أَرۡضِكُم بِسِحۡرِهِۦ فَمَاذَا تَأۡمُرُونَ
Anataka kuwatoa nyinyi, kwa uchawi wake, kwenye ardhi yenu. Basi mnatoa shauri gani kuhusu yeye nipate kuyafuata maoni yenu?»
અરબી તફસીરો:
قَالُوٓاْ أَرۡجِهۡ وَأَخَاهُ وَٱبۡعَثۡ فِي ٱلۡمَدَآئِنِ حَٰشِرِينَ
Watu wake wakamwambia, «Msubirishe Mūsā na Hārūn, na utume askari mijini wawakusanye wachawi.
અરબી તફસીરો:
يَأۡتُوكَ بِكُلِّ سَحَّارٍ عَلِيمٖ
Watakujia na kila anayejua uchawi na akawa hodari kuufahamu.»
અરબી તફસીરો:
فَجُمِعَ ٱلسَّحَرَةُ لِمِيقَٰتِ يَوۡمٖ مَّعۡلُومٖ
Wakakusanywa wachawi, na wakapangiwa wakati maalumu, nao ni wakati wa mchana wa siku ya Pambo ambayo wanajitenga na shughuli zao, na wanajikusanya na kujipamba, ili wakutane na Mūsā
અરબી તફસીરો:
وَقِيلَ لِلنَّاسِ هَلۡ أَنتُم مُّجۡتَمِعُونَ
na wawahimize watu kujumuika kwa matarajio kwamba ushindi uwe ni wa wachawi.
અરબી તફસીરો:
لَعَلَّنَا نَتَّبِعُ ٱلسَّحَرَةَ إِن كَانُواْ هُمُ ٱلۡغَٰلِبِينَ
Sisi tunatarajia ushindi uwe ni wa wachawi ili tujikite kwenye dini yetu.
અરબી તફસીરો:
فَلَمَّا جَآءَ ٱلسَّحَرَةُ قَالُواْ لِفِرۡعَوۡنَ أَئِنَّ لَنَا لَأَجۡرًا إِن كُنَّا نَحۡنُ ٱلۡغَٰلِبِينَ
Na wachawi walipomjia Fir’awn walimwambia, ‘Je, sisi tutakuwa na malipo ya mali au heshima ikiwa tutakuwa ni wenye kumshinda Mūsā?»
અરબી તફસીરો:
قَالَ نَعَمۡ وَإِنَّكُمۡ إِذٗا لَّمِنَ ٱلۡمُقَرَّبِينَ
Fir’awn akasema, «Ndio, nyinyi mtapata kwangu malipo mnayoyataka, na nyinyi hapo mtakuwa ni miongoni mwa wenye kusogezwa karibu na mimi.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ لَهُم مُّوسَىٰٓ أَلۡقُواْ مَآ أَنتُم مُّلۡقُونَ
Mūsā akasema kuwaambia wachawi, akitaka kuutangua uchawi wao na kuonyesha kuwa kile alichokileta si uchawi, «Tupeni mtakavyovitupa vya uchawi.»
અરબી તફસીરો:
فَأَلۡقَوۡاْ حِبَالَهُمۡ وَعِصِيَّهُمۡ وَقَالُواْ بِعِزَّةِ فِرۡعَوۡنَ إِنَّا لَنَحۡنُ ٱلۡغَٰلِبُونَ
Basi wakatupa kamba zao na fimbo zao, na zikawadhihirikia watu kwenye akili zao kuwa ni nyoka wanaotembea, na wakaapa kwa enzi ya Fir’awn kwa kusema, «Sisi ni wenye kushinda.»
અરબી તફસીરો:
فَأَلۡقَىٰ مُوسَىٰ عَصَاهُ فَإِذَا هِيَ تَلۡقَفُ مَا يَأۡفِكُونَ
Hapo akaitupa Mūsā fimbo yake, na papo hapo ikawa ni nyoka mkubwa, akawa anavimeza vile vilivyotokana na wao, hao wachawi, vya uzushi na bandia.
અરબી તફસીરો:
فَأُلۡقِيَ ٱلسَّحَرَةُ سَٰجِدِينَ
Waliposhuhudia hilo na wakajua kuwa halitokani na udanganyifu wa wachawi, walimuamini Mwenyezi Mungu na wakamsujudia
અરબી તફસીરો:
قَالُوٓاْ ءَامَنَّا بِرَبِّ ٱلۡعَٰلَمِينَ
na wakasema, «Tumemuamini Mola wa viumbe vyote,
અરબી તફસીરો:
رَبِّ مُوسَىٰ وَهَٰرُونَ
Mola wa Mūsā na Hārūn.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ ءَامَنتُمۡ لَهُۥ قَبۡلَ أَنۡ ءَاذَنَ لَكُمۡۖ إِنَّهُۥ لَكَبِيرُكُمُ ٱلَّذِي عَلَّمَكُمُ ٱلسِّحۡرَ فَلَسَوۡفَ تَعۡلَمُونَۚ لَأُقَطِّعَنَّ أَيۡدِيَكُمۡ وَأَرۡجُلَكُم مِّنۡ خِلَٰفٖ وَلَأُصَلِّبَنَّكُمۡ أَجۡمَعِينَ
Fir’awn akasema kuwaambia wachawi kwa kukataa, «Mumemkubali Mūsā bila ya idhini yangu!» Na akasema akiashiria kuwa kitendo cha Mūsā ni uchawi, «Yeye ni mkubwa wenu aliyewafundisha nyinyi uchawi, basi mtayajua mateso yatakayowafikia. Nitaikata mikono yenu na miguu yenu kitafauti: kwa kuukata mkono wa kulia na mguu wa kushoto au kinyume chake, na nitawasulubu nyote.»
અરબી તફસીરો:
قَالُواْ لَا ضَيۡرَۖ إِنَّآ إِلَىٰ رَبِّنَا مُنقَلِبُونَ
Wachawi walisema kumwambia Fir’awn, «Hakuna madhara ya duniani yatakayotupata, kwa kweli sisi ni wenye kurudi kwa Mola wetu, Atupe neema ya kuendelea.
અરબી તફસીરો:
إِنَّا نَطۡمَعُ أَن يَغۡفِرَ لَنَا رَبُّنَا خَطَٰيَٰنَآ أَن كُنَّآ أَوَّلَ ٱلۡمُؤۡمِنِينَ
Sisi tunataraji Mola wetu Atusamehe makosa yetu ya ushirikina na mengineyo kwa kuwa sisi ndio Waumini wa mwanzo katika watu wako.»
અરબી તફસીરો:
۞ وَأَوۡحَيۡنَآ إِلَىٰ مُوسَىٰٓ أَنۡ أَسۡرِ بِعِبَادِيٓ إِنَّكُم مُّتَّبَعُونَ
Na Mwenyezi Mungu Akampelekea wahyi Mūsā, amani imshukie, kwamba, «Enda usiku pamoja na walioamini miongoni mwa Wana wa Isrāīl, ili Fir’awn na askari wake, ambao watawafuata nyinyi, wasije wakawafikia kabla ya kufika kwenu baharini.»
અરબી તફસીરો:
فَأَرۡسَلَ فِرۡعَوۡنُ فِي ٱلۡمَدَآئِنِ حَٰشِرِينَ
Fir’awn akawatuma askari wake, alipopata habari kwamba Wana wa Isrāīl wameenda usiku, wakusanye jeshi lake kutoka miji ya utawala wake.
અરબી તફસીરો:
إِنَّ هَٰٓؤُلَآءِ لَشِرۡذِمَةٞ قَلِيلُونَ
Fir’awn akasema, «Kwa kweli, Wana wa Isrāīl waliokimbia pamoja na Mūsā ni pote twevu lenye idadi ndogo.
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّهُمۡ لَنَا لَغَآئِظُونَ
Na wao wamevijaza hasira vifua vyetu kwa kuwa wameenda kinyume na dini yetu na wametoka bila ya idhini yetu,
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّا لَجَمِيعٌ حَٰذِرُونَ
na sisi sote tuko macho, tuko tayari nao.»
અરબી તફસીરો:
فَأَخۡرَجۡنَٰهُم مِّن جَنَّٰتٖ وَعُيُونٖ
Mwenyezi Mungu Akamtoa Fir’awn na watu wake kwenye ardhi ya Misri yenye mabustani, mabubujiko ya maji,
અરબી તફસીરો:
وَكُنُوزٖ وَمَقَامٖ كَرِيمٖ
hazina za mali na majumba mazuri.
અરબી તફસીરો:
كَذَٰلِكَۖ وَأَوۡرَثۡنَٰهَا بَنِيٓ إِسۡرَٰٓءِيلَ
Na kama tulivyowatoa, tuliwapatia nyumba hizo Wana wa Isrāīl baada yao wao.
અરબી તફસીરો:
فَأَتۡبَعُوهُم مُّشۡرِقِينَ
Hivyo basi Fir’awn na askari wake walimkuta Mūsā na waliokuwa pamoja na yeye wakati wa kuchomoza jua.
અરબી તફસીરો:
فَلَمَّا تَرَٰٓءَا ٱلۡجَمۡعَانِ قَالَ أَصۡحَٰبُ مُوسَىٰٓ إِنَّا لَمُدۡرَكُونَ
Yalipoonana makundi mawili, watu wa Mūsā walisema, «Kwa hakika jumuiko la Fir’awn ni lenye kutufikia na kutuangamiza.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ كَلَّآۖ إِنَّ مَعِيَ رَبِّي سَيَهۡدِينِ
Mūsā alisema kuwaambia, «Sivyo! Mambo si kama mlivyotaja. Hamtafikiwa. Kwa hakika Mwenyezi Mungu Yupo na mimi kwa msaada, Ataniongoza njia ya kuokoka mimi na kuokoka nyinyi.»
અરબી તફસીરો:
فَأَوۡحَيۡنَآ إِلَىٰ مُوسَىٰٓ أَنِ ٱضۡرِب بِّعَصَاكَ ٱلۡبَحۡرَۖ فَٱنفَلَقَ فَكَانَ كُلُّ فِرۡقٖ كَٱلطَّوۡدِ ٱلۡعَظِيمِ
Hapo tukampelekea wahyi Mūsā kwamba, «Piga bahari kwa fimbo yako!» Akapiga. Na bahari ikapasuka njia kumi na mbili kwa idadi ya kabila za Wana wa Isrāīl. Na kila kipande kilichojitenga na bahari ni kama jabali kubwa.
અરબી તફસીરો:
وَأَزۡلَفۡنَا ثَمَّ ٱلۡأٓخَرِينَ
Na tulimsogeza karibu Fir’awn na watu wake mpaka wakaingia baharini.
અરબી તફસીરો:
وَأَنجَيۡنَا مُوسَىٰ وَمَن مَّعَهُۥٓ أَجۡمَعِينَ
Na tukamuokoa Mūsā na waliokuwa pamoja na yeye wote. Bahari ikaendelea kuachana kwake (kwa ule mpasuko) mpaka wakavuka kwenye nchi kavu.
અરબી તફસીરો:
ثُمَّ أَغۡرَقۡنَا ٱلۡأٓخَرِينَ
Kisha tukamzamisha Fir’awn na waliokuwa pamoja na yeye kwa kuifanya bahari iwafinike baada ya wao kuingia ndani wakimfuata Mūsā na watu wake.
અરબી તફસીરો:
إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَأٓيَةٗۖ وَمَا كَانَ أَكۡثَرُهُم مُّؤۡمِنِينَ
Kwa hakika, katika hilo lililotukia pana mazingatio ya ajabu yenye kuonyesha dalili ya uweza wa Mwenyezi Mungu. Na wengi wa wafuasi wa Fir’awn hawakuwa ni wenye kuamini, pamoja na alama hii yenye kushinda.
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ ٱلۡعَزِيزُ ٱلرَّحِيمُ
Na hakika ya Mola wako Ndiye Mshindi, Ndiye Mwenye kurehemu. Kwa nguvu Zake na ushindi Amewaangamiza makafiri wakanushaji, na kwa rehema Yake Amemuokoa Mūsā na waliokuwa pamoja na yeye wote.
અરબી તફસીરો:
وَٱتۡلُ عَلَيۡهِمۡ نَبَأَ إِبۡرَٰهِيمَ
Na wasimulie makafiri, ewe Mtume, habari ya Ibrāhīm
અરબી તફસીરો:
إِذۡ قَالَ لِأَبِيهِ وَقَوۡمِهِۦ مَا تَعۡبُدُونَ
alipomwambia babake na watu wake, «Mnaabudu kitu gani?»
અરબી તફસીરો:
قَالُواْ نَعۡبُدُ أَصۡنَامٗا فَنَظَلُّ لَهَا عَٰكِفِينَ
Wakasema, «Tunaabudu masanamu, tunaketi na kuendelea kuwaabudu.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ هَلۡ يَسۡمَعُونَكُمۡ إِذۡ تَدۡعُونَ
Akasema Ibrāhīm akiwatanabahisha uharibifu wa njia yao, «Kwani wanasikia maombi yenu mnapowaomba?
અરબી તફસીરો:
أَوۡ يَنفَعُونَكُمۡ أَوۡ يَضُرُّونَ
Au wanawapatia manufaa mkiwaabudu? Au wanawafanya mupate madhara mkiacha kuwaabudu?»
અરબી તફસીરો:
قَالُواْ بَلۡ وَجَدۡنَآ ءَابَآءَنَا كَذَٰلِكَ يَفۡعَلُونَ
Wakasema, «Haliwi lolote katika hayo, lakini tuliwakuta mababa zetu wakiwaabudu, na sisi tukawaiga katika yale ambayo walikuwa wakiyafanya.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ أَفَرَءَيۡتُم مَّا كُنتُمۡ تَعۡبُدُونَ
Ibrāhīm akasema, «Je, mumefikiria kuvitia akilini hivyo mnavyoviabudu, miongoni mwa masanamu yasiyosikia wala kunufaisha wala kudhuru,
અરબી તફસીરો:
أَنتُمۡ وَءَابَآؤُكُمُ ٱلۡأَقۡدَمُونَ
nyinyi na mababa zenu waliowatangulia?
અરબી તફસીરો:
فَإِنَّهُمۡ عَدُوّٞ لِّيٓ إِلَّا رَبَّ ٱلۡعَٰلَمِينَ
Kwani hao mnaowaabudu badala ya Mwenyezi Mungu ni maadui zangu. Lakini Mola wa viumbe wote na Mmiliki wa mambo yao, Yeye Peke Yake Ndiye ninayemuabudu.
અરબી તફસીરો:
ٱلَّذِي خَلَقَنِي فَهُوَ يَهۡدِينِ
Yeye Ndiye Aliyeniumba kwa sura nzuri zaidi. Yeye ananiongoza kwenye maslahi ya dunia na Akhera.
અરબી તફસીરો:
وَٱلَّذِي هُوَ يُطۡعِمُنِي وَيَسۡقِينِ
Na Yeye Ndiye Anayenineemesha kwa chakula na kinywaji.
અરબી તફસીરો:
وَإِذَا مَرِضۡتُ فَهُوَ يَشۡفِينِ
Na nikipatikana na ugonjwa, Yeye Ndiye Anayeniponyesha na kuniondolea.
અરબી તફસીરો:
وَٱلَّذِي يُمِيتُنِي ثُمَّ يُحۡيِينِ
Na Yeye Ndiye Atakayenifisha duniani kwa kuichukua roho yangu, kisha Atanihuisha Siku ya Kiyama, hakuna awezaye hilo isipokuwa Yeye.
અરબી તફસીરો:
وَٱلَّذِيٓ أَطۡمَعُ أَن يَغۡفِرَ لِي خَطِيٓـَٔتِي يَوۡمَ ٱلدِّينِ
Na Ambaye ninatarajia Atanisamehe dhambi zangu Siku ya Malipo.»
અરબી તફસીરો:
رَبِّ هَبۡ لِي حُكۡمٗا وَأَلۡحِقۡنِي بِٱلصَّٰلِحِينَ
Ibrāhīm akasema akimuomba Mola wake, «Mola wangu! Nitunukie elimu na fahamu, na unikutanishe na watu wema, na unikusanye mimi na wao Peponi.
અરબી તફસીરો:
وَٱجۡعَل لِّي لِسَانَ صِدۡقٖ فِي ٱلۡأٓخِرِينَ
«Na unifanye niwe na sifa nzuri na utajo mwema kwa wale watakaokuja baada yangu mpaka Siku ya Kiyama.
અરબી તફસીરો:
وَٱجۡعَلۡنِي مِن وَرَثَةِ جَنَّةِ ٱلنَّعِيمِ
«Na unifanye mimi niwe miongoni mwa waja wako utakaowarithisha starehe za Peponi.»
અરબી તફસીરો:
وَٱغۡفِرۡ لِأَبِيٓ إِنَّهُۥ كَانَ مِنَ ٱلضَّآلِّينَ
Hii ni dua ya Ibrāhīm, amani imshukiye, ya kumuomba Mwenyezi Mungu Amuokoe babake na upotevu na Ampe uongofu, ili Amghufirie na Amsamehe, kama Ibrāhīm alivyomuahidi babake kumuombea Mungu, na ilipomfunukia kuwa yeye ni mwenye kuendelea kwenye ukafiri na ushirikina mpaka afe alijiepusha naye.
અરબી તફસીરો:
وَلَا تُخۡزِنِي يَوۡمَ يُبۡعَثُونَ
«Na usinipe unyonge Siku hiyo, ambayo watu watatoka makaburini ili wahesabiwe na walipwe,
અરબી તફસીરો:
يَوۡمَ لَا يَنفَعُ مَالٞ وَلَا بَنُونَ
Siku ambayo mali na watoto havitamfaa yoyote miongoni mwa waja,
અરબી તફસીરો:
إِلَّا مَنۡ أَتَى ٱللَّهَ بِقَلۡبٖ سَلِيمٖ
isipokuwa yule aliyemjia Mwenyezi Mungu kwa moyo uliyosalimika na ukafiri, unafiki na uovu.»
અરબી તફસીરો:
وَأُزۡلِفَتِ ٱلۡجَنَّةُ لِلۡمُتَّقِينَ
Na Pepo itasogezwa karibu kwa wale waliojiepusha na ukafiri na matendo ya uasi na wakamuelekea Mwenyezi Mungu kwa kumtii.
અરબી તફસીરો:
وَبُرِّزَتِ ٱلۡجَحِيمُ لِلۡغَاوِينَ
Na Moto utaonyeshwa waziwazi kwa makafiri ambao walipotea njia ya uongofu na wakayafanyia ujasiri yaliyoharamishwa na Mwenyezi Mungu na wakawakanusha Mitume Wake.
અરબી તફસીરો:
وَقِيلَ لَهُمۡ أَيۡنَ مَا كُنتُمۡ تَعۡبُدُونَ
Na wataambiwa kwa kulaumiwa, «Wako wapi waungu wenu ambao mlikuwa mkiwaabudu
અરબી તફસીરો:
مِن دُونِ ٱللَّهِ هَلۡ يَنصُرُونَكُمۡ أَوۡ يَنتَصِرُونَ
badala ya Mwenyezi Mungu na mkidai kwamba wao watawaombea leo? Je, watawanusuru na wawazuilie adhabu isiwafikie au watajinusuru kwa kuikinga adhabu isiwafikie?» Hakuna chochote katika hayo.
અરબી તફસીરો:
فَكُبۡكِبُواْ فِيهَا هُمۡ وَٱلۡغَاوُۥنَ
Hapo watakusanywa na watupwe kwenye Jahanamu kwa vichwa vyao, mara baada ya nyingine mpaka watakapotulia humo: wao, wale waliowapoteza
અરબી તફસીરો:
وَجُنُودُ إِبۡلِيسَ أَجۡمَعُونَ
na wasaidizi wa Iblisi waliowapambia shari; hakuna yoyote kati yao atakayeponyoka.
અરબી તફસીરો:
قَالُواْ وَهُمۡ فِيهَا يَخۡتَصِمُونَ
Watasema wakikiri makosa yao, na huku wanagombana, ndani ya Jahanamu, na wale waliowapoteza wao,
અરબી તફસીરો:
تَٱللَّهِ إِن كُنَّا لَفِي ضَلَٰلٖ مُّبِينٍ
«Tunaapa kwa Mwenyezi Mungu kwamba sisi, duniani, tulikuwa kwenye upotevu ulio waziwazi, haukuwa umefichika,
અરબી તફસીરો:
إِذۡ نُسَوِّيكُم بِرَبِّ ٱلۡعَٰلَمِينَ
tulipowafanya nyinyi kuwa ni sawa na Mola wa viumbe wote, Anayestahiki kuabudiwa, Peke Yake.
અરબી તફસીરો:
وَمَآ أَضَلَّنَآ إِلَّا ٱلۡمُجۡرِمُونَ
Na hakuna kilichotutia kwenye mwisho huu mbaya isipokuwa ni wahalifu ambao walitulingania tumuabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu.
અરબી તફસીરો:
فَمَا لَنَا مِن شَٰفِعِينَ
«Hapana yoyote wa kutuombea na kututoa kwenye adhabu
અરબી તફસીરો:
وَلَا صَدِيقٍ حَمِيمٖ
wala mwenye kutupenda kikweli na kutuhurumia.
અરબી તફસીરો:
فَلَوۡ أَنَّ لَنَا كَرَّةٗ فَنَكُونَ مِنَ ٱلۡمُؤۡمِنِينَ
«Tunatamani tupatiwe fursa ya kurudi ulimwenguni tupate kuwa miongoni mwa wenye kuamini na kuokolewa.»
અરબી તફસીરો:
إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَأٓيَةٗۖ وَمَا كَانَ أَكۡثَرُهُم مُّؤۡمِنِينَ
Hakika katika habari ya Ibrāhīm iliyotangulia kuna mazingatio kwa mwenye kuzingatia. Na wengi wenye kuisikia habari hii hawakuwa ni wenye kuamini.
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ ٱلۡعَزِيزُ ٱلرَّحِيمُ
Na kwa hakika, Mola wako Ndiye Mshindi Aliye Muweza wa kuwalipiza wakanushaji, Ndiye Mwenye kuwarehemu waja Wake Waumini.
અરબી તફસીરો:
كَذَّبَتۡ قَوۡمُ نُوحٍ ٱلۡمُرۡسَلِينَ
Waliukanusha watu wa Nūḥ ujumbe wa Nabii wao. Wakawa, kwa kufanya hivyo, ni wakanushaji wa Mitume wote, kwa kuwa kila Mtume anaamrisha kuwaamini Mitume wote.
અરબી તફસીરો:
إِذۡ قَالَ لَهُمۡ أَخُوهُمۡ نُوحٌ أَلَا تَتَّقُونَ
Kumbuka pindi aliposema kuwaambia wao ndugu yao Nūḥ, «Je, hamumuogopi Mwenyezi Mungu kwa kuacha kumuabudu asiyekuwa Yeye?
અરબી તફસીરો:
إِنِّي لَكُمۡ رَسُولٌ أَمِينٞ
Mimi kwenu nyinyi ni Mtume muaminifu katika yale ninayowafikishia.
અરબી તફસીરો:
فَٱتَّقُواْ ٱللَّهَ وَأَطِيعُونِ
Basi ifanyeni Imani kuwa ndio kinga yenu na adhabu ya Mwenyezi Mungu, na nitiini mimi katika yale ninayowaamrisha ya kumuabudu Yeye Peke Yake,
અરબી તફસીરો:
وَمَآ أَسۡـَٔلُكُمۡ عَلَيۡهِ مِنۡ أَجۡرٍۖ إِنۡ أَجۡرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ ٱلۡعَٰلَمِينَ
na sitaki kutoka kwenu malipo yoyote ya kuufikisha ujumbe, malipo yangu hayako juu ya yoyote isipokuwa Mola wa viumbe wote, Mwenye kuendesha mambo ya viumbe Vyake.
અરબી તફસીરો:
فَٱتَّقُواْ ٱللَّهَ وَأَطِيعُونِ
Basi jihadharini na mateso Yake na mnitii mimi kwa kufuata amri Zake na kujiepusha na makatazo Yake.»
અરબી તફસીરો:
۞ قَالُوٓاْ أَنُؤۡمِنُ لَكَ وَٱتَّبَعَكَ ٱلۡأَرۡذَلُونَ
Watu wake wakamwambia, «Vipi tutakuamini na tutakufuata na hali hao waliokufuata ni watu wanyonge na wale wa hali ya chini miongoni mwao?»
અરબી તફસીરો:
قَالَ وَمَا عِلۡمِي بِمَا كَانُواْ يَعۡمَلُونَ
Nūḥ, amani imshukie, aliwajibu kwa kusema, «Sikupewa jukumu la kujua matendo yao. Jukumu nililopewa ni kuwalingania wao kwenye Imani. Na linalozingatiwa ni Imani, na sio cheo, ukoo, kazi na ujuzi wa sanaa.
અરબી તફસીરો:
إِنۡ حِسَابُهُمۡ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّيۖ لَوۡ تَشۡعُرُونَ
«Hesabu yao, ili walipwe kwa matendo yao na yaliyomo ndani ya nafsi zao, ni juu ya Mola wangu Anayeona na kujua siri zote. Lau mnatambua hilo hamngalisema maneno haya.
અરબી તફસીરો:
وَمَآ أَنَا۠ بِطَارِدِ ٱلۡمُؤۡمِنِينَ
«Na mimi si mwenye kuwafukuza wale wanaouamini ulinganizi wangu, namna itakavyokuwa hali yao, kwa kufuata matakwa yenu, ili mniamini.
અરબી તફસીરો:
إِنۡ أَنَا۠ إِلَّا نَذِيرٞ مُّبِينٞ
Mimi sikuwa isipokuwa ni mwonyaji ambaye onyo lake liko wazi.»
અરબી તફસીરો:
قَالُواْ لَئِن لَّمۡ تَنتَهِ يَٰنُوحُ لَتَكُونَنَّ مِنَ ٱلۡمَرۡجُومِينَ
Hapo watu wa Nūḥ waliacha kubishana na wakaamua kutoa vitisho, hivyo basi wakamuambia, «Usiporudi nyuma, ewe Nūḥ, ukaacha huo ulinganizi wako, utakuwa ni miongoni mwa wenye kuuawa kwa kupigwa mawe.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ رَبِّ إِنَّ قَوۡمِي كَذَّبُونِ
Nūḥ aliposikia neno lao hili, alimuomba Mola wake kwa kusema, «Mola wangu! Kwa hakika watu wangu wameamua kuendelea kunikanusha,
અરબી તફસીરો:
فَٱفۡتَحۡ بَيۡنِي وَبَيۡنَهُمۡ فَتۡحٗا وَنَجِّنِي وَمَن مَّعِيَ مِنَ ٱلۡمُؤۡمِنِينَ
basi amua baina yangu na wao uamuzi wa kumwangamiza mwenye kukataa kukupwekesha na akamkanusha Mtume wako. Na uniokoe mimi, na Waumini walio pamoja na mimi, na adhabu utakayowaadhibu makafiri.»
અરબી તફસીરો:
فَأَنجَيۡنَٰهُ وَمَن مَّعَهُۥ فِي ٱلۡفُلۡكِ ٱلۡمَشۡحُونِ
Basi tukamuokoa na wale walio pamoja na yeye katika jahazi iliyojazwa aina mbalimabali za viumbe alivyovibeba pamoja na yeye.
અરબી તફસીરો:
ثُمَّ أَغۡرَقۡنَا بَعۡدُ ٱلۡبَاقِينَ
Kisha tukawazamisha, baada ya kumuokoa Nūḥ na wale waliokuwa pamoja na yeye, wale waliosalia kati ya wale ambao hawakuamini na wakaukataa ushauri aliyowapa.
અરબી તફસીરો:
إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَأٓيَةٗۖ وَمَا كَانَ أَكۡثَرُهُم مُّؤۡمِنِينَ
Hakika katika maelezo ya Nūḥ na yale yaliyokuwa ya kuokolewa Waumini na kuangamizwa wakanushaji ni alama na ni zingatio kubwa kwa waliokuja baada yao. Na wengi wa wale waliokisikia kisa hiki hawakuwa ni wenye kumuamini Mwenyezi Mungu, Mtume Wake na sheria Zake.
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ ٱلۡعَزِيزُ ٱلرَّحِيمُ
Na kwa kweli Mola wako Ndiye Mshindi katika kuwatesa waliomkanusha na wakaenda kinyume na amri Yake, Mwenye rehema kwa waja Wake walioamini.
અરબી તફસીરો:
كَذَّبَتۡ عَادٌ ٱلۡمُرۡسَلِينَ
Walimkanusha watu wa kabila la ‘Ād Mtume wao Hūd, amani imshukiye, na kwa hivyo wakawa ni wakanushaji wa Mitume wote, kwa kuwa ulinganizi wao ni mmoja katika misingi yake na malengo yake.
અરબી તફસીરો:
إِذۡ قَالَ لَهُمۡ أَخُوهُمۡ هُودٌ أَلَا تَتَّقُونَ
Alipowaambia ndugu yao Hūd, «Je, hamumchi MwenyeziMungu mukamtakasia ibada?
અરબી તફસીરો:
إِنِّي لَكُمۡ رَسُولٌ أَمِينٞ
Mimi nimetumwa kwenu niwaongoze na niwaonyeshe njia, ni mtunzi wa ujumbe wa Mwenyezi Mungu, ninaufikisha kwenu kama Alivyoniamrisha Mola wangu.
અરબી તફસીરો:
فَٱتَّقُواْ ٱللَّهَ وَأَطِيعُونِ
Basi iogopeni adhabu ya Mwenyezi Mungu na mnitii mimi katika kile ninachowaitia nyinyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu,
અરબી તફસીરો:
وَمَآ أَسۡـَٔلُكُمۡ عَلَيۡهِ مِنۡ أَجۡرٍۖ إِنۡ أَجۡرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ ٱلۡعَٰلَمِينَ
na sitaki kutoka kwenu, kwa kuwaongoza nyinyi kwenye kumpwekesha Mwenyezi Mungu, aina yoyote ya malipo. Malipo yangu hayako juu ya yoyote isipokuwa Mola wa viumbe wote.
અરબી તફસીરો:
أَتَبۡنُونَ بِكُلِّ رِيعٍ ءَايَةٗ تَعۡبَثُونَ
«Je mnajenga kila mahali palipoinuka jengo refu mkawa mnatazama kutoka hapo na mnawacheza shere wapita njia? Huo ni upuuzi na upitaji kiasi, na hauwaletei nyinyi faida yoyote katika dini au katika dunia.
અરબી તફસીરો:
وَتَتَّخِذُونَ مَصَانِعَ لَعَلَّكُمۡ تَخۡلُدُونَ
Na mnafanya majumba imara na ngome zilizojengwa madhubuti, kama kwamba nyinyi mtakaa milele duniani na hamtakufa.
અરબી તફસીરો:
وَإِذَا بَطَشۡتُم بَطَشۡتُمۡ جَبَّارِينَ
Na mnapomshika mtu kwa nguvu na mkamakinika kumuua au kumpiga, basi mnalifanya hilo kwa kutendesha nguvu hali ya kufanya maonevu.
અરબી તફસીરો:
فَٱتَّقُواْ ٱللَّهَ وَأَطِيعُونِ
«Basi muogopeni Mwenyezi Mungu na mkifuate kile ninachowalingania, kwani hilo lina nafuu zaidi kwenu,
અરબી તફસીરો:
وَٱتَّقُواْ ٱلَّذِيٓ أَمَدَّكُم بِمَا تَعۡلَمُونَ
na mcheni Mwenyezi Mungu Aliyewapa aina mbalimbali za neema zisizofichika kwenu.
અરબી તફસીરો:
أَمَدَّكُم بِأَنۡعَٰمٖ وَبَنِينَ
Amewapa wanyama hawa: ngamia ng’ombe, mbuzi na kondoo, na Amewapa watoto,
અરબી તફસીરો:
وَجَنَّٰتٖ وَعُيُونٍ
na Amewapa mabustani yenye matunda, na Amewatolea maji kwenye chemchemi zinazopita.
અરબી તફસીરો:
إِنِّيٓ أَخَافُ عَلَيۡكُمۡ عَذَابَ يَوۡمٍ عَظِيمٖ
Hūd, amani imshukiye, akasema akiwatahadharisha wao, «Mimi ninaogopa , mkiendelea na yale mliyo nayo ya ukanushaji, uonevu na kuzikufuru neema, asije Mwenyezi Mungu Akawateremshia nyinyi adhabu katika Siku ambayo shida yake ni kubwa kwa kitisho cha adhabu yake.
અરબી તફસીરો:
قَالُواْ سَوَآءٌ عَلَيۡنَآ أَوَعَظۡتَ أَمۡ لَمۡ تَكُن مِّنَ ٱلۡوَٰعِظِينَ
Wakamwambia, «Ni sawa kwetu kutukumbusha, kututisha na kuacha kufanya hivyo, hatutakuamini.
અરબી તફસીરો:
إِنۡ هَٰذَآ إِلَّا خُلُقُ ٱلۡأَوَّلِينَ
Na wakasema, «Haikuwa dini hii tuliyonayo isipokuwa ni dini ya watu wa mwanzo na desturi zao,
અરબી તફસીરો:
وَمَا نَحۡنُ بِمُعَذَّبِينَ
na sisi si wenye kuadhibiwa kwa tunalolifanya katika yale ambayo unatuonya nayo ya adhabu.»
અરબી તફસીરો:
فَكَذَّبُوهُ فَأَهۡلَكۡنَٰهُمۡۚ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَأٓيَةٗۖ وَمَا كَانَ أَكۡثَرُهُم مُّؤۡمِنِينَ
Wakaendelea kumkanusha, na Mwenyezi Mungu Akawaangamiza kwa upepo wa baridi ulio mkali. Kwa hakika, katika kuangamiza huko kuna mazingatio kwa wanaokuja baada yao, na hawakuwa wengi wao, wale waliokisikia kisa chao, ni wenye kukuamini wewe.
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ ٱلۡعَزِيزُ ٱلرَّحِيمُ
Hakika Mola wako Ndiye Mwenye nguvu, Mshindi kwa anayoyataka ya kuwaangamiza wakanushaji, Mwenye huruma kwa Waumini.
અરબી તફસીરો:
كَذَّبَتۡ ثَمُودُ ٱلۡمُرۡسَلِينَ
Watu wa kabila la Thamūd waliukanusha ujumbe wa Mtume wao Ṣāliḥ na wakaukanusha mwito wake wa kumpwekesha Mwenyezi Mungu, na kwa hivyo wakawa wamewakanusha Mitume wote, kwa kuwa wao wote wanalingania kwenye kumpwekesha Mwenyezi Mungu.
અરબી તફસીરો:
إِذۡ قَالَ لَهُمۡ أَخُوهُمۡ صَٰلِحٌ أَلَا تَتَّقُونَ
Pindi alipowaambia wao ndugu yao Ṣāliḥ»Je, hamuogopi mateso ya Mwenyezi Mungu, mkampwekesha kwa ibada?
અરબી તફસીરો:
إِنِّي لَكُمۡ رَسُولٌ أَمِينٞ
Mimi nimetumilizwa kwenu kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ni mwenye kuutunza ujumbe huu kama nilivyoupokea kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
અરબી તફસીરો:
فَٱتَّقُواْ ٱللَّهَ وَأَطِيعُونِ
Basi jihadharini na mateso Yake, Aliyetukuka, na fuateni kile nilichowalingania mkifuate.
અરબી તફસીરો:
وَمَآ أَسۡـَٔلُكُمۡ عَلَيۡهِ مِنۡ أَجۡرٍۖ إِنۡ أَجۡرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ ٱلۡعَٰلَمِينَ
Na mimi sitaki malipo kwa kuwashauri na kuwaongoza, malipo yangu hayako isipokuwa kwa Mola wa viumbe wote.
અરબી તફસીરો:
أَتُتۡرَكُونَ فِي مَا هَٰهُنَآ ءَامِنِينَ
«Je, Awaache Mola wenu katika starehe mlizonazo, hali ya kuwa mumetulia katika dunia hii mkiwa mumesalimika na adhabu na kuondoka na kufa?
અરબી તફસીરો:
فِي جَنَّٰتٖ وَعُيُونٖ
Mkiwa kwenye mabustani yenye matunda, chemchemi zinazopita,
અરબી તફસીરો:
وَزُرُوعٖ وَنَخۡلٖ طَلۡعُهَا هَضِيمٞ
nafaka nyingi na mitende ambayo matunda yake yamestawi, yamelainika na yameiva,
અરબી તફસીરો:
وَتَنۡحِتُونَ مِنَ ٱلۡجِبَالِ بُيُوتٗا فَٰرِهِينَ
na mnachonga kutoka kwa majabali majumba hali ya kuwa ni wamahiri wa kuyachonga, mkiwa na kiburi na majivuno.»
અરબી તફસીરો:
فَٱتَّقُواْ ٱللَّهَ وَأَطِيعُونِ
Basi ogopeni adhabu ya Mwenyezi Mungu na mkubali ushauri wangu,
અરબી તફસીરો:
وَلَا تُطِيعُوٓاْ أَمۡرَ ٱلۡمُسۡرِفِينَ
na msiandame amri ya wenye kuzidhulumu nafsi zao, waliokolea katika kumuasi Mwenyezi Mungu,
અરબી તફસીરો:
ٱلَّذِينَ يُفۡسِدُونَ فِي ٱلۡأَرۡضِ وَلَا يُصۡلِحُونَ
waliozoea kufanya uharibifu kwenye ardhi, uharibifu usiotengenezeka.
અરબી તફસીરો:
قَالُوٓاْ إِنَّمَآ أَنتَ مِنَ ٱلۡمُسَحَّرِينَ
Watu wa Thamūd walimwambia Nabii wao Ṣāliḥ, «Wewe hukuwa isipokuwa ni miongoni mwa wale waliofanyiwa uganga wa uchawi mwingi, mpaka uchawi ukaathiri akili yako.
અરબી તફસીરો:
مَآ أَنتَ إِلَّا بَشَرٞ مِّثۡلُنَا فَأۡتِ بِـَٔايَةٍ إِن كُنتَ مِنَ ٱلصَّٰدِقِينَ
Hukuwa wewe isipokuwa ni mmoja wa wanadamu unaofanana na sisi katika ubinadamu, basi vipi utakuwa tafauti na sisi kwa utume? Basi leta hoja wazi inayoonyesha kuwa utume wako umethibiti, iwapo wewe ni mkweli katika madai yako kwamba Mwenyezi Mungu Amekutumiliza kwetu.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ هَٰذِهِۦ نَاقَةٞ لَّهَا شِرۡبٞ وَلَكُمۡ شِرۡبُ يَوۡمٖ مَّعۡلُومٖ
Ṣāliḥ akasema kuwaambia- na hapo alikuwa amewaletea ngamia ambaye Mwenyezi Mungu alimtolea kwenye jiwe-, «Huyu ni ngamia wa Mwenyezi Mungu. Yeye ana hisa ya maji siku maalumu, na nyinyi mna hisa ya maji kwa siku nyingine. Haifai kwenu nyinyi kunywa siku ile ambayo ni hisa yake, na yeye hatakunywa siku ambayo ni hisa yenu.
અરબી તફસીરો:
وَلَا تَمَسُّوهَا بِسُوٓءٖ فَيَأۡخُذَكُمۡ عَذَابُ يَوۡمٍ عَظِيمٖ
Na msimguse kwa kitu chochote cha kumdhuru, kama kipigo au mauaji au mfano wake, kwani mkifanya hivyo, Mwenyezi Mungu Atawaangamiza nyinyi kwa adhabu ya Siku ambayo shida yake ni kubwa kwa sababu ya papatiko litakalotukia Siku hiyo na shida.
અરબી તફસીરો:
فَعَقَرُوهَا فَأَصۡبَحُواْ نَٰدِمِينَ
Basi wakamchinja ngamia, wakawa ni wenye kujuta kwa walilolifanya walipokuwa na uhakika kuwa watashukiwa na adhabu, na majuto yao yasiwafae kitu.
અરબી તફસીરો:
فَأَخَذَهُمُ ٱلۡعَذَابُۚ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَأٓيَةٗۖ وَمَا كَانَ أَكۡثَرُهُم مُّؤۡمِنِينَ
Basi adhabu ya Mwenyezi Mungu ikawashukia, ile ambayo Ṣāliḥ, amani imshukiye, aliwaahidi nayo, na ikawaangamiza. Kwa hakika, katika kuwaangamiza watu wa Thamūd pana mazingatio kwa mwenye kuuzingatia mwisho huu; na wengi wao hawakuwa ni wenye kuamini.
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ ٱلۡعَزِيزُ ٱلرَّحِيمُ
Na kwa hakika Mola wako Ndiye Mshindi, Mwenye kutendesha nguvu, Mwenye kuwatesa maadui Wake, Mwenye huruma kwa walioamini miongoni mwa viumbe Wake.
અરબી તફસીરો:
كَذَّبَتۡ قَوۡمُ لُوطٍ ٱلۡمُرۡسَلِينَ
watu wa Lūṭ waliukanusha utume wake, wakawa kwa hilo ni wakanushaji wa Mitume waliosalia, kwa kuwa lile walilolileta la kumpwekesha Mwenyezi Mungu na misingi ya Sheria ni moja.
અરબી તફસીરો:
إِذۡ قَالَ لَهُمۡ أَخُوهُمۡ لُوطٌ أَلَا تَتَّقُونَ
Pindi ndugu yao Lūṭ alipowaambia, «Je, hamuogopi adhabu ya Mwenyezi Mungu?
અરબી તફસીરો:
إِنِّي لَكُمۡ رَسُولٌ أَمِينٞ
Mimi ni mjumbe kutoka kwa Mola wenu aliye muaminifu juu ya utekelezaji wa ujumbe Wake kwenu.
અરબી તફસીરો:
فَٱتَّقُواْ ٱللَّهَ وَأَطِيعُونِ
Basi jihadharini na mateso ya Mwenyezi Mungu kwa kumkanusha kwenu mjumbe Wake, na nifuateni mimi katika yale ninayowalingania.
અરબી તફસીરો:
وَمَآ أَسۡـَٔلُكُمۡ عَلَيۡهِ مِنۡ أَجۡرٍۖ إِنۡ أَجۡرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ ٱلۡعَٰلَمِينَ
Na siwaombi malipo yoyote juu ya ulinganizi wangu wa kuwaongoza, malipo yangu hayako isipokuwa kwa Mola wa viumbe wote.
અરબી તફસીરો:
أَتَأۡتُونَ ٱلذُّكۡرَانَ مِنَ ٱلۡعَٰلَمِينَ
«Mnawaingilia binadamu wanaume
અરબી તફસીરો:
وَتَذَرُونَ مَا خَلَقَ لَكُمۡ رَبُّكُم مِّنۡ أَزۡوَٰجِكُمۚ بَلۡ أَنتُمۡ قَوۡمٌ عَادُونَ
na mnawaacha wake zenu ambao Mwenyezi Mungu Amewaumbia nyinyi ili mstarehe na mzaane? Lakini nyinyi ni watu, kwa uasi huu, wenye kuyakiuka yale ambayo Mwenyezi Mungu Amewaruhusu ya halali na kuyaendea ya haramu.»
અરબી તફસીરો:
قَالُواْ لَئِن لَّمۡ تَنتَهِ يَٰلُوطُ لَتَكُونَنَّ مِنَ ٱلۡمُخۡرَجِينَ
Watu wa Lūṭ wakasema, «Usipoacha, ewe Lūṭ, kutukataza kuwajia wanaume na kukichafua kitendo hicho (cha kuwajia wanaume), utakuwa ni miongoni mwa wenye kufukuzwa kutoka miji yetu.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ إِنِّي لِعَمَلِكُم مِّنَ ٱلۡقَالِينَ
Lūṭ akasema kuwaambia wao, «Mimi ni miongoni mwa wale wanaokichukia sana kitendo chenu mnachokifanya cha kuwajia wanaume.»
અરબી તફસીરો:
رَبِّ نَجِّنِي وَأَهۡلِي مِمَّا يَعۡمَلُونَ
Kisha Lūṭ akamuomba Mola wake, alipokata tamaa kuwa watamsikiliza, alisema, «Mola wangu! Niokoe mimi na uwaokoe jamaa zangu na kile wanachokifanya watu wangu cha uasi huu mchafu na (utuokoe na) adhabu yako itakayowapata.»
અરબી તફસીરો:
فَنَجَّيۡنَٰهُ وَأَهۡلَهُۥٓ أَجۡمَعِينَ
Basi tukamuokoa yeye na watu wa nyumbani kwake na wale wote walioukubali ulinganizi wake,
અરબી તફસીરો:
إِلَّا عَجُوزٗا فِي ٱلۡغَٰبِرِينَ
isipokuwa mkongwe miongoni mwa watu wa nyumbani kwake, naye ni mke wake ambaye hakushirikiana na wao katika kuamini, hivyo basi akawa ni mwenye kusalia kwenye adhabu na maangamivu.
અરબી તફસીરો:
ثُمَّ دَمَّرۡنَا ٱلۡأٓخَرِينَ
Kisha tukawaangamiza wasiokuwa wao, miongoni mwa makafiri, kuwaangamiza kukubwa,
અરબી તફસીરો:
وَأَمۡطَرۡنَا عَلَيۡهِم مَّطَرٗاۖ فَسَآءَ مَطَرُ ٱلۡمُنذَرِينَ
na tukawateremshia wao mawe kutoka juu kama mvua yakawaangamiza. Ilikuwa mvua mbaya sana ya wale walioonywa na Mitume wao na wasiwakubalie. Kwa hakika, wao wameteremshiwa aina mabaya zaidi za maangamivu na uvunjaji.
અરબી તફસીરો:
إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَأٓيَةٗۖ وَمَا كَانَ أَكۡثَرُهُم مُّؤۡمِنِينَ
Kwa hakika, katika mateso hayo yaliyowateremkia watu wa Lūṭ pana mazingatio na mawaidha ya kuwafanya wenye kukanusha wawaidhike. Na wengi wao hawakuwa ni wenye kuamini.
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ ٱلۡعَزِيزُ ٱلرَّحِيمُ
Na kwa kweli Mola wako Ndiye Mshindi Mwenye nguvu ya kuweza kuwashurutisha wakanushaji, Mwenye huruma kwa waja Wake wema.
અરબી તફસીરો:
كَذَّبَ أَصۡحَٰبُ لۡـَٔيۡكَةِ ٱلۡمُرۡسَلِينَ
Walimkanusha watu wa nchi yenye miti iliyoshikana Mtume wao Shu’ayb kuhusu utume wake, na kwa hivyo waliukua wamekanusha jumbe zote za Mitume.
અરબી તફસીરો:
إِذۡ قَالَ لَهُمۡ شُعَيۡبٌ أَلَا تَتَّقُونَ
Alipowaambia wao Shu’ayb, «Je, hamuogopi kuwa Mwenyezi Mungu Atawatesa kwa ushirikina wenu na kufanya kwenu matendo ya uasi?
અરબી તફસીરો:
إِنِّي لَكُمۡ رَسُولٌ أَمِينٞ
Mimi nimetumilizwa kwenu kutoka kwa Mwenyezi Mungu niwaongoe, ni mtunzi wa kile alichoniletea mimi Mwenyezi Mungu cha wahyi wa utume.
અરબી તફસીરો:
فَٱتَّقُواْ ٱللَّهَ وَأَطِيعُونِ
Basi yaogopeni mateso ya Mwenyezi Mungu na mkifuate kile ninachowaitia cha uongofu wa Mwenyezi Mungu mupate kuongoka.
અરબી તફસીરો:
وَمَآ أَسۡـَٔلُكُمۡ عَلَيۡهِ مِنۡ أَجۡرٍۖ إِنۡ أَجۡرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ ٱلۡعَٰلَمِينَ
Na sitaki kwenu, kwa kule kuwalingania kwangu kwenye kumuamini Mwenyezi Mungu, malipo yoyote. Malipo yangu hayako isipokuwa kwa Mola wa viumbe wote.”
અરબી તફસીરો:
۞ أَوۡفُواْ ٱلۡكَيۡلَ وَلَا تَكُونُواْ مِنَ ٱلۡمُخۡسِرِينَ
Shu’ayb akaendelea kuwaambia- na walikuwa wakipunguza vipimo na mizani-, «Watimizieni watu vipimo kwa kuwakamilishia, na msiwe ni kati ya wale wanaowapunja watu haki zao,
અરબી તફસીરો:
وَزِنُواْ بِٱلۡقِسۡطَاسِ ٱلۡمُسۡتَقِيمِ
na mpime kwa mizani ya uadilifu iliyolingana sawa,
અરબી તફસીરો:
وَلَا تَبۡخَسُواْ ٱلنَّاسَ أَشۡيَآءَهُمۡ وَلَا تَعۡثَوۡاْ فِي ٱلۡأَرۡضِ مُفۡسِدِينَ
na msiwapunje watu chochote katika haki zao kwenye vipimo au mizani au vinginevyo, na msizidishe uharibifu katika ardhi kwa kufanya ushirikina, kuua, kunyang’anya, kuwatisha watu na kutekeleza vitendo vya uasi.
અરબી તફસીરો:
وَٱتَّقُواْ ٱلَّذِي خَلَقَكُمۡ وَٱلۡجِبِلَّةَ ٱلۡأَوَّلِينَ
«Na jihadharini na mateso ya Mwenyezi Mungu Aliyewaumba na Akawaumba watu wa mataifa yaliyowatangulia.»
અરબી તફસીરો:
قَالُوٓاْ إِنَّمَآ أَنتَ مِنَ ٱلۡمُسَحَّرِينَ
Wakasema, «Ukweli ni kwamba wewe, ewe Shu’ayb, ni miongoni mwa wale waliopatwa na uchawi ukawashika sana ukawaondoa akili zao.
અરબી તફસીરો:
وَمَآ أَنتَ إِلَّا بَشَرٞ مِّثۡلُنَا وَإِن نَّظُنُّكَ لَمِنَ ٱلۡكَٰذِبِينَ
Na wewe hukuwa isipokuwa ni mfano wetu sisi katika ubinadamu, basi vipi utahusika peke yako kwa utume bila ya sisi? Na kwa kweli, dhana yetu kubwa kuhusu wewe ni kuwa wewe ni miongoni mwa warongo katika kile unachokidai cha utume.
અરબી તફસીરો:
فَأَسۡقِطۡ عَلَيۡنَا كِسَفٗا مِّنَ ٱلسَّمَآءِ إِن كُنتَ مِنَ ٱلصَّٰدِقِينَ
Iwapo wewe ni mkweli katika madai yako ya utume, basi muombe Mwenyezi Mungu Atuangushie vipande vya adhabu kutoka mbinguni vitumalize.»
અરબી તફસીરો:
قَالَ رَبِّيٓ أَعۡلَمُ بِمَا تَعۡمَلُونَ
Shu’ayb akawaambia wao, «Mola wangu Anayajua zaidi yale mnayoyafanya ya ushirikina na uasi na mateso mnayostahili.»
અરબી તફસીરો:
فَكَذَّبُوهُ فَأَخَذَهُمۡ عَذَابُ يَوۡمِ ٱلظُّلَّةِۚ إِنَّهُۥ كَانَ عَذَابَ يَوۡمٍ عَظِيمٍ
Wakaendelea kumkanusha, likawapata wao joto kali, wakawa wanatafuta mahali pa hifadhi ili wajifinike. Kikawafinika kiwingu, kikawapatia ubaridi na upepo laini, na walipokusanyika chini yake, moto uliwawakia na ukawachoma, basi hapo yakawa maangamivu yao wote katika siku yenye kitisho kikali.
અરબી તફસીરો:
إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَأٓيَةٗۖ وَمَا كَانَ أَكۡثَرُهُم مُّؤۡمِنِينَ
Hakika katika mateso hayo yaliyowashukia kuna ushahidi wazi juu ya uweza wa Mwenyezi Mungu katika kuwapatiliza wakanushaji kwa adhabu na kuna mazingatio kwa mwenye kuzingatia. Na hawakuwa wengi wao ni wenye kuamini na kuwaidhika kwa hayo.
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ ٱلۡعَزِيزُ ٱلرَّحِيمُ
Na kwa hakika, Mola wako, ewe Mtume, Ndiye Yeye Aliye Mshindi katika kuwatesa Kwake wale Anaowatesa miongoni mwa maadui Wake, Ndiye Anayewarehemu waja Wake wanaompwekesha.
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّهُۥ لَتَنزِيلُ رَبِّ ٱلۡعَٰلَمِينَ
Na kwa hakika, hii Qur’ani ambayo ndani yake zimetajwa habari hizi za kweli imeteremshwa na Muumba viumbe na Mmiliki wa mambo yote.
અરબી તફસીરો:
نَزَلَ بِهِ ٱلرُّوحُ ٱلۡأَمِينُ
Jibrili muaminifu ameshuka nayo
અરબી તફસીરો:
عَلَىٰ قَلۡبِكَ لِتَكُونَ مِنَ ٱلۡمُنذِرِينَ
akakusomea mpaka ukaikusanya moyoni mwako, kwa kuihifadhi na kuielewa, upate kuwa ni mmoja wa wajumbe wa Mwenyezi Mungu wenye kuwafanya watu wao waogope mateso ya Mwenyezi Mungu, upate kuwaonya, kwa Teremsho hili, binadamu na majini wote.
અરબી તફસીરો:
بِلِسَانٍ عَرَبِيّٖ مُّبِينٖ
Ameshuka nayo Jibrili kwako kwa lugha ya Kiarabu yenye maana yaliyo wazi, yenye ushahidi unaoonekena, ikikusanya kile wanachokihitajia cha kutengeneza mambo ya Dini yao na dunia yao.
અરબી તફસીરો:
وَإِنَّهُۥ لَفِي زُبُرِ ٱلۡأَوَّلِينَ
Na kwa hakika, utajo wa hii Qur’ani umethibitishwa katika Vitabu vya Manabii waliotangulia, vimeibashiri na kukubali kuwa ni ya kweli.
અરબી તફસીરો:
أَوَلَمۡ يَكُن لَّهُمۡ ءَايَةً أَن يَعۡلَمَهُۥ عُلَمَٰٓؤُاْ بَنِيٓ إِسۡرَٰٓءِيلَ
Je, haiwatoshi hawa kuwa ni ushahidi kwamba wewe ni mtume wa Mwenyezi Mungu na kwamba Qur’ani ni kweli kuwa wasomi wa Wana wa Isrāīl wana ujuzi wa usahihi wa hilo na wale walioamini miongoni mwao kama ‘Abdullāh bin Sallām?
અરબી તફસીરો:
وَلَوۡ نَزَّلۡنَٰهُ عَلَىٰ بَعۡضِ ٱلۡأَعۡجَمِينَ
Na lau tungaliiteremsha Qur’ani kwa baadhi ya wale wasiozungumza lugha ya Kiarabu
અરબી તફસીરો:
فَقَرَأَهُۥ عَلَيۡهِم مَّا كَانُواْ بِهِۦ مُؤۡمِنِينَ
wakawasomea makafiri wa Kikureshi kisomo cha Kiarabu kilicho sawa, wangaliikanusha pia na wangalizua sababu ya ukanushaji wao.
અરબી તફસીરો:
كَذَٰلِكَ سَلَكۡنَٰهُ فِي قُلُوبِ ٱلۡمُجۡرِمِينَ
Hivyo ndivyo tulivyotia ndani ya nyoyo za wahalifu kuikanusha Qur’ani na hilo likawa limejikita ndani ya hizo nyoyo,
અરબી તફસીરો:
لَا يُؤۡمِنُونَ بِهِۦ حَتَّىٰ يَرَوُاْ ٱلۡعَذَابَ ٱلۡأَلِيمَ
na hii ikawa ni sababu ya udhalimu wao na uhalifu wao. Basi hapana njia ya wao kubadilika kwa kuyaacha waliyonayo ya kuikanusha Qur’ani mpaka waishuhudie adhabu kali walioahidiwa.
અરબી તફસીરો:
فَيَأۡتِيَهُم بَغۡتَةٗ وَهُمۡ لَا يَشۡعُرُونَ
Hapo adhabu iwashukie ghafla na hali wao hawajui kuja kwake kabla ya hapo,
અરબી તફસીરો:
فَيَقُولُواْ هَلۡ نَحۡنُ مُنظَرُونَ
na hapo waseme, watakaposhtushwa nayo, kwa majuto ya Imani iliyotupita tukaikosa, «Je, sisi ni wenye kupatiwa nafasi na kucheleweshwa tupate kutubia kwa Mwenyezi Mungu ushirikina wetu na tuyapatilize yaliyotupita?»
અરબી તફસીરો:
أَفَبِعَذَابِنَا يَسۡتَعۡجِلُونَ
Je, hawa wamedanganyika na kule kuwapa muhula kwangu ndipo wakawa wanataka kuteremka adhabu kwa haraka juu yao kutoka mbinguni?
અરબી તફસીરો:
أَفَرَءَيۡتَ إِن مَّتَّعۡنَٰهُمۡ سِنِينَ
Je, umejua, ewe Mtume, lau tungaliwastarehesha kwa uhai wa miaka mingi kwa kuwacheleweshea muda wao wa kuishi
અરબી તફસીરો:
ثُمَّ جَآءَهُم مَّا كَانُواْ يُوعَدُونَ
kisha iwashukie adhabu ilioahidiwa?
અરબી તફસીરો:
مَآ أَغۡنَىٰ عَنۡهُم مَّا كَانُواْ يُمَتَّعُونَ
Hakutawafaa kitu kule kustarehe kwao kwa umri mrefu na maisha mazuri wasipotubia kutokana na ushirikina wao. Basi adhabu ya Mwenyezi Mungu ni yenye kuwashukia hivi karibuni (ulimwenguni) au baadaye (huko Akhera).
અરબી તફસીરો:
وَمَآ أَهۡلَكۡنَا مِن قَرۡيَةٍ إِلَّا لَهَا مُنذِرُونَ
Na hatukuuangamiza mji wowote, miongoni mwa miji katika mataifa yote, isipokuwa baada ya kuwatumiliza Mitume kwao wawaonye,
અરબી તફસીરો:
ذِكۡرَىٰ وَمَا كُنَّا ظَٰلِمِينَ
ili wawe ni makumbusho kwao na uzindushi wa yale yenye uokofu kwao. Na hatukuwa ni wenye kudhulumu kwa kuwaadhibu watu kabla ya kuwapelekea Mtume.
અરબી તફસીરો:
وَمَا تَنَزَّلَتۡ بِهِ ٱلشَّيَٰطِينُ
Na Qur’ani hawakuiteremsha mashetani kwa Muhammad, kama wanavyodai makafiri,
અરબી તફસીરો:
وَمَا يَنۢبَغِي لَهُمۡ وَمَا يَسۡتَطِيعُونَ
na hilo halifai kutoka kwao na wala hawaliwezi,
અરબી તફસીરો:
إِنَّهُمۡ عَنِ ٱلسَّمۡعِ لَمَعۡزُولُونَ
kwa kuwa wao ni wenye kuzuiliwa kuisikiliza Qur’ani kutoka mbinguni, ni wenye kupigwa na vimondo.
અરબી તફસીરો:
فَلَا تَدۡعُ مَعَ ٱللَّهِ إِلَٰهًا ءَاخَرَ فَتَكُونَ مِنَ ٱلۡمُعَذَّبِينَ
Hivyo basi usiabudu, pamoja na Mwenyezi Mungu, muabudiwa yoyote asiyekuwa Yeye, ufanyapo hivyo utateremkiwa na adhabu ile iliyowashukia hawa walioabudu, pamoja na Mwenyezi Mungu, asiyekuwa Yeye.
અરબી તફસીરો:
وَأَنذِرۡ عَشِيرَتَكَ ٱلۡأَقۡرَبِينَ
Na watahadharishe, ewe Muhammad, watu wako wa karibu, ukianzia na wale walio karibu na wewe zaidi, isije adhabu yetu ikawashukia.
અરબી તફસીરો:
وَٱخۡفِضۡ جَنَاحَكَ لِمَنِ ٱتَّبَعَكَ مِنَ ٱلۡمُؤۡمِنِينَ
Na uwe laini wa mwenendo na maneno, kwa unyenyekevu na huruma, kwa yule ambaye imekufunukia kutoka kwake kuitika mwito wako.
અરબી તફસીરો:
فَإِنۡ عَصَوۡكَ فَقُلۡ إِنِّي بَرِيٓءٞ مِّمَّا تَعۡمَلُونَ
Basi wakienda kinyume na amri yako na wasikufuate, jiepushe na vitendo vyao na yale waliyonayo ya ushirikina na upotevu.
અરબી તફસીરો:
وَتَوَكَّلۡ عَلَى ٱلۡعَزِيزِ ٱلرَّحِيمِ
Na Umuachie jambo lako Mwenyezi Mungu, Aliye Mshindi Ambaye hakuna wa kushindana na Yeye wala wa kumlazimisha, Mwenye kurehemu Ambaye Hawaachi wenye kumtegemea.
અરબી તફસીરો:
ٱلَّذِي يَرَىٰكَ حِينَ تَقُومُ
Na Ambaye Anakuona unaposimama kuswali ukiwa peke yako ndani ya usiku.
અરબી તફસીરો:
وَتَقَلُّبَكَ فِي ٱلسَّٰجِدِينَ
Na Anaona vile unavyogeuka, pamoja na wenye kumsujudia katika Swala zao wakiwa na wewe, ukiwa katika hali ya kusimama, kurukuu na kusujudu na kuketi.
અરબી તફસીરો:
إِنَّهُۥ هُوَ ٱلسَّمِيعُ ٱلۡعَلِيمُ
Hakika Yeye, kutakasika na sifa za upungufu ni Kwake, Ndiye Anayesikia kusoma kwako na kumtaja kwako, Ndiye Anayejua nia yako na matendo yako.
અરબી તફસીરો:
هَلۡ أُنَبِّئُكُمۡ عَلَىٰ مَن تَنَزَّلُ ٱلشَّيَٰطِينُ
Je, niwapashe habari, enyi watu, ni nani ambaye mashetani wanamshukia?
અરબી તફસીરો:
تَنَزَّلُ عَلَىٰ كُلِّ أَفَّاكٍ أَثِيمٖ
Wanamshukia kila mwingi wa urongo, mwingi wa madhambi miongoni mwa makuhani.
અરબી તફસીરો:
يُلۡقُونَ ٱلسَّمۡعَ وَأَكۡثَرُهُمۡ كَٰذِبُونَ
Mashetani wanasikiliza kwa kuiba, wanayanyakuwa maneno kutoka sehemu za juu wakawatupia makuhani na wale wanaokuwa na mwenendo wao miongoni mwa watu wenye matendo mabaya. Na wengi wa hawa ni warongo, kwani mmoja wao husema kweli katika neno moja na akaongeza juu yake maneno mia moja ya urongo.
અરબી તફસીરો:
وَٱلشُّعَرَآءُ يَتَّبِعُهُمُ ٱلۡغَاوُۥنَ
Na washairi, mashairi yao yanasimama juu ya ubatilifu na urongo, na wanafuatana na wao wapotevu waliopotoka kama wao.
અરબી તફસીરો:
أَلَمۡ تَرَ أَنَّهُمۡ فِي كُلِّ وَادٖ يَهِيمُونَ
Kwani huoni, ewe Nabii, kwamba wao wanaenda kama mtu aliyekosa mwelekeo, wanavama ndani ya kila aina ya fani za urongo, uzushi, uvunjaji heshima, kutukana nasaba na kuwataja vibaya wanawake waliojihifadhi,
અરબી તફસીરો:
وَأَنَّهُمۡ يَقُولُونَ مَا لَا يَفۡعَلُونَ
na kwamba wao wanayasema wasiyoyatenda, wanapita mipaka katika kuwasifu watu wa ubatilifu na wanawatia kasoro watu wa haki.
અરબી તફસીરો:
إِلَّا ٱلَّذِينَ ءَامَنُواْ وَعَمِلُواْ ٱلصَّٰلِحَٰتِ وَذَكَرُواْ ٱللَّهَ كَثِيرٗا وَٱنتَصَرُواْ مِنۢ بَعۡدِ مَا ظُلِمُواْۗ وَسَيَعۡلَمُ ٱلَّذِينَ ظَلَمُوٓاْ أَيَّ مُنقَلَبٖ يَنقَلِبُونَ
Mwenyezi Mungu amewavua, kati ya hao washairi, wale washairi walioongoka kwa kuamini na kufanya matendo mema, na wakamtaja Mwenyezi Mungu kwa wingi, wakatunga mashairi juu ya kumpwekesha Mwenyezi Mungu, kutakata na sifa za upungufu ni Kwake, na kumsifu Yeye, Mwenye utajo mtukufu, na kumtetea Mtume Wake, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie, wakasema maneno ya busara yenye mawaidha na adabu nzuri, na wakaunusuru Uislamu wakawa wanamtukana anayeutukana au anayemtukana Mtume wake kwa kuwarudi washairi makafiri. Na watajua wale waliozidhulumu nafsi zao kwa ushirikina na matendo ya uasi, wakawadhulumu wasiokuwa wao kwa kuwanyima haki zao au kuwafanyia uadui au tuhuma za urongo, ni marejeo gani ya shari na maangamivu watakayorejea. Kwa kweli, hayo ni mageuko mabaya. Tunamuomba Mwenyezi Mungu salama na afya.
અરબી તફસીરો:
 
શબ્દોનું ભાષાંતર સૂરહ: અશ્ શુઅરાઅ
સૂરહ માટે અનુક્રમણિકા પેજ નંબર
 
કુરઆન મજીદના શબ્દોનું ભાષાંતર - સવાહિલી ભાષાતર - અબ્દુલ્લાહ મુહમ્મદ અને નાસિર ખમીસ - ભાષાંતરોની અનુક્રમણિકા

સ્વાહિલી ભાષામાં કુરઆન મજીદનું ભાષાતર, ભાષાતર કરનારનું નામ અદ્ દૂકતુર અબ્દુલ્લાહ મુહમ્મદ અબૂ બકર અને શેખ નાસીર ખમીસ

બંધ કરો