Prijevod značenja časnog Kur'ana - الترجمة السواحلية - عبد الله محمد وناصر خميس * - Sadržaj prijevodā


Prijevod značenja Sura: Sura eš-Šura   Ajet:

Surat Ash-Shura

حمٓ
«Ḥā, Mīm,
Tefsiri na arapskom jeziku:
عٓسٓقٓ
'Ayn, Sīn, Qāf» Yametangulia maelezo juu ya herufi zilizokatwa na kutengwa mwanzo wa sura ya Al-Baqarah.
Tefsiri na arapskom jeziku:
كَذَٰلِكَ يُوحِيٓ إِلَيۡكَ وَإِلَى ٱلَّذِينَ مِن قَبۡلِكَ ٱللَّهُ ٱلۡعَزِيزُ ٱلۡحَكِيمُ
Kama Alivyokuteremshia Mwenyezi Mungu, ewe Nabii, hii Qur’ani, Aliteremsha Vitabu na Kurasa kwa Manabii kabla yako. Na Yeye Ndiye Mshindi katika kutesa Kwake, Ndiye Mwenye hekima katika maneno Yake na vitendo Vyake.
Tefsiri na arapskom jeziku:
لَهُۥ مَا فِي ٱلسَّمَٰوَٰتِ وَمَا فِي ٱلۡأَرۡضِۖ وَهُوَ ٱلۡعَلِيُّ ٱلۡعَظِيمُ
Ni vya Mwenyezi Mungu Peke Yake vilivyoko mbinguni na ardhini, na Yeye Ndiye wa juu kwa cheo Chake na utendeshaji nguvu Wake, Aliye Mkuu Ambaye Ana ukubwa na enzi.
Tefsiri na arapskom jeziku:
تَكَادُ ٱلسَّمَٰوَٰتُ يَتَفَطَّرۡنَ مِن فَوۡقِهِنَّۚ وَٱلۡمَلَٰٓئِكَةُ يُسَبِّحُونَ بِحَمۡدِ رَبِّهِمۡ وَيَسۡتَغۡفِرُونَ لِمَن فِي ٱلۡأَرۡضِۗ أَلَآ إِنَّ ٱللَّهَ هُوَ ٱلۡغَفُورُ ٱلرَّحِيمُ
Zinakaribia mbingu kupasuka- pasuka, kila moja juu ya ile inayoifuata, kutokana na ukubwa wa Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema na haiba Yake, Mwingi wa fadhila na utukufu, na hali Malaika wanamtakasia Shukurani Mola wao na kumwepusha na kila sifa ambayo hanasibiani nayo, na wanamuomba Mola wao msamaha wa dhambi za waliyoko ardhini miongoni mwa wale wanaomuamini. Jueni mtanabahi kwamba Mwenyezi Mungu Ndiye Mwenye kusamehe sana dhambi za waja Wake Waumini na Ndiye Mwenye kuwarehemu.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَٱلَّذِينَ ٱتَّخَذُواْ مِن دُونِهِۦٓ أَوۡلِيَآءَ ٱللَّهُ حَفِيظٌ عَلَيۡهِمۡ وَمَآ أَنتَ عَلَيۡهِم بِوَكِيلٖ
Na wale waliowafanya wasiokuwa Mwenyezi Mungu kuwa ni waungu badala Yake wakawategemea na kuwaabudu, basi Mwenyezi Mungu Anavidhibiti vitendo vyao, ili Awalipe kwavyo Siku ya Kiyama. Na wewe hukuwakilishwa kuvidhibiti vitendo vyao. Hakika yako wewe ni muonyaji tu, hivyo basi ni juu yako kufikisha na ni juu yetu kuhesabu.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَكَذَٰلِكَ أَوۡحَيۡنَآ إِلَيۡكَ قُرۡءَانًا عَرَبِيّٗا لِّتُنذِرَ أُمَّ ٱلۡقُرَىٰ وَمَنۡ حَوۡلَهَا وَتُنذِرَ يَوۡمَ ٱلۡجَمۡعِ لَا رَيۡبَ فِيهِۚ فَرِيقٞ فِي ٱلۡجَنَّةِ وَفَرِيقٞ فِي ٱلسَّعِيرِ
Na kama tulivyowapelekea wahyi Manabii kabla yako wewe, tulikuletea wahyi wa Qur’ani iliyo kwa lugha ya Kiarabu, ili uwaonye watu wa Makkah na watu wote wengine pambizoni mwake[9], na uwaonye Siku ya Mkusanyiko, nayo ni Siku ya Kiyama, ambayo kuja kwake hakuna shaka, ambapo watu Siku hiyo watakuwa mapote mawili: pote moja litakuwa Peponi, nalo ni lile la waliomuamini Mwenyezi Mungu na wakayafuata yale aliyokuja nayo Mtume Wake Muhammad, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie, na pote lingine litakuwa Motoni, nalo ni lile la waliomkanusha Mwenyezi Mungu na wakaenda kinyume na yale aliyokuja nayo Mtume Wake, Muhammad, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie.
[9]Kwa kuwa Makkah ni kituo cha ardhi Umm al Qurā (Mama wa miji) kwa kuwu ni mji mtukufu kuliko miji yote, ndio ikawa miji yote mingine pamoja na watu wake huwa imeizunguka Makkah na iko pambizoni mwake. Utukufu wa Makkah juu ya sehemu zote za ardhi pia umithibiti kwenye hadithi za Mtum (s.a.w). Ang. Tafsiri ya Ibn Kathīr katika kufasiri aya hii: 42 :7.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَلَوۡ شَآءَ ٱللَّهُ لَجَعَلَهُمۡ أُمَّةٗ وَٰحِدَةٗ وَلَٰكِن يُدۡخِلُ مَن يَشَآءُ فِي رَحۡمَتِهِۦۚ وَٱلظَّٰلِمُونَ مَا لَهُم مِّن وَلِيّٖ وَلَا نَصِيرٍ
Na lau Angalitaka Mwenyezi Mungu Kuwakusanya viumbe Wake kwenye uongofu na kuwafanya wawe kwenye mila moja iliyoongoka angalifanya hivyo, lakini Yeye Anataka kuwatia kwenye rehema Yake Anaowataka miongoni mwa waja Wake. Na wale wenye kuzidhulumu nafsi zao kwa kufanya ushirikina, basi hao hawatakuwa na yoyote wa kumtegemea atakayesimamia mambo yao Siku ya Kiyama, wala msaidizi atakayewanusuru kutokana na adhabu ya Mwenyezi Mungu Aliyetukuka.
Tefsiri na arapskom jeziku:
أَمِ ٱتَّخَذُواْ مِن دُونِهِۦٓ أَوۡلِيَآءَۖ فَٱللَّهُ هُوَ ٱلۡوَلِيُّ وَهُوَ يُحۡيِ ٱلۡمَوۡتَىٰ وَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيۡءٖ قَدِيرٞ
Bali hawa washirikina waliwachukuwa wasiokuwa Mwenyezi Mungu kuwa ni wategemewa wakawa wanawategemea. Mwenyezi Mungu Peke Yake Ndiye Mwenye kutegemewa, mja anamtegemea kwa kumuabudu na kumtii, na Yeye Anawasimamia waja Wake Waumini kwa kuwatoa kwenye giza kuwatia kwenye mwangaza na kwa kuwasaidia katika mambo yao yote. Na Yeye Anahuisha waliokufa wakati wa kufufuliwa, na Yeye kwa kila jambo ni Mweza, hakuna chochote kinachomshinda.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَمَا ٱخۡتَلَفۡتُمۡ فِيهِ مِن شَيۡءٖ فَحُكۡمُهُۥٓ إِلَى ٱللَّهِۚ ذَٰلِكُمُ ٱللَّهُ رَبِّي عَلَيۡهِ تَوَكَّلۡتُ وَإِلَيۡهِ أُنِيبُ
Na kitu chochote kile mnachotafautiana kwacho , enyi watu, miongoni mwa mambo ya dini yenu, basi hukumu irudishwe kwa Mwenyezi Mungu katika Kitabu Chake na Sunnah ya Mtume Wake, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie. Huyo Ndiye Mwenyezi Mungu, Mola wangu na Mola wenu, Kwake Yeye nimetegemea katika mambo yangu, na Kwake Yeye ninarejea katika hali zangu zote.
Tefsiri na arapskom jeziku:
فَاطِرُ ٱلسَّمَٰوَٰتِ وَٱلۡأَرۡضِۚ جَعَلَ لَكُم مِّنۡ أَنفُسِكُمۡ أَزۡوَٰجٗا وَمِنَ ٱلۡأَنۡعَٰمِ أَزۡوَٰجٗا يَذۡرَؤُكُمۡ فِيهِۚ لَيۡسَ كَمِثۡلِهِۦ شَيۡءٞۖ وَهُوَ ٱلسَّمِيعُ ٱلۡبَصِيرُ
Mwenyezi Mungu, kutakasika ni Kwake na kutukuka ni Kwake, Ndiye Muumba mbingu na ardhi na Muanzilishi wa kuzitengeneza kwa uweza Wake na matakwa Yake na hekima Yake. Amewapatia nyinyi wake wanaotokana na nyinyi ili mjitulize kwao, na Amewapatia nyinyi wanyama-howa wa kila aina, wa kiume na wa kike. Anawafanya nyinyi muwe wengi kwa kuzaana kwa njia hii ya kutangamana. Hakuna kinachofanana na Yeye, Aliyetukuka, na kuwa kama Yeye chochote kile miongoni mwa viumbe vyake, si katika dhati Yake wala majina Yake wala sifa Zake wala vitendo Vyake. Kwani majina Yake yote ni mazuri na sifa Zake ni sifa za ukamilifu na utukufu; na kwa vitendo Vyake, Aliyetukuka, Amefanya vipatikane viumbe vikubwa bila ya kuwa na mshirika. Na Yeye Ndiye Mwenye kusikia na Ndiye Mwenye kuona. Hakuna chochote kinachofichamana Kwake cha matendo ya waja Wake na maneno yao, na Atawalipa kwa hayo.
Tefsiri na arapskom jeziku:
لَهُۥ مَقَالِيدُ ٱلسَّمَٰوَٰتِ وَٱلۡأَرۡضِۖ يَبۡسُطُ ٱلرِّزۡقَ لِمَن يَشَآءُ وَيَقۡدِرُۚ إِنَّهُۥ بِكُلِّ شَيۡءٍ عَلِيمٞ
Ni Wake Yeye, kutakasika ni Kwake, ufalme wa mbinguni na ardhini, na mkononi Mwake kuna funguo za rehema na riziki, Anamkunjulia riziki Yake Anayemtaka miongoni mwa waja Wake na Anambania Anayemtaka. Hakika Yeye , Aliyetukuka na kuwa juu, ni Mjuzi wa kila kitu, Hakifichamani Kwake Yeye chochote katika mambo ya viumbe Vyake.
Tefsiri na arapskom jeziku:
۞ شَرَعَ لَكُم مِّنَ ٱلدِّينِ مَا وَصَّىٰ بِهِۦ نُوحٗا وَٱلَّذِيٓ أَوۡحَيۡنَآ إِلَيۡكَ وَمَا وَصَّيۡنَا بِهِۦٓ إِبۡرَٰهِيمَ وَمُوسَىٰ وَعِيسَىٰٓۖ أَنۡ أَقِيمُواْ ٱلدِّينَ وَلَا تَتَفَرَّقُواْ فِيهِۚ كَبُرَ عَلَى ٱلۡمُشۡرِكِينَ مَا تَدۡعُوهُمۡ إِلَيۡهِۚ ٱللَّهُ يَجۡتَبِيٓ إِلَيۡهِ مَن يَشَآءُ وَيَهۡدِيٓ إِلَيۡهِ مَن يُنِيبُ
Amewawekea nyinyi, enyi watu, Sheria ya Dini tuliyokuletea kwa njia ya wahyi, ewe Mtume, nayo ni Uislamu, na ile Aliyomuusia Nūḥ aifuate kivitendo na aifikishe kwa watu, na ile aliyowausia Ibrāhīm, Mūsā na Īsā (Watano hawa ndio Ulū al- 'azm [wenye hima] miongoni mwa Mitume kulingana na kauli iliyo mashuhuri) kwamba msimamishe Dini kwa kumpwekesha Mwenyezi Mungu, kumtii na kumuabudu Yeye na sio mwingine, na msitafautiane katika Dini ambayo nimewaamrisha muifuate. Ni kubwa mno juu ya washirikina lile mnalowalingania la kumpwekesha Mwenyezi Mungu na kumtakasia ibada. Mwenyezi Mungu Anamchagua Anayemtaka miongoni mwa viumbe Vyake awe ni mwenye kumpwekesha na Anamuongoza yule anayerejea Kwake afanye matendo ya utiifu Kwake.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَمَا تَفَرَّقُوٓاْ إِلَّا مِنۢ بَعۡدِ مَا جَآءَهُمُ ٱلۡعِلۡمُ بَغۡيَۢا بَيۡنَهُمۡۚ وَلَوۡلَا كَلِمَةٞ سَبَقَتۡ مِن رَّبِّكَ إِلَىٰٓ أَجَلٖ مُّسَمّٗى لَّقُضِيَ بَيۡنَهُمۡۚ وَإِنَّ ٱلَّذِينَ أُورِثُواْ ٱلۡكِتَٰبَ مِنۢ بَعۡدِهِمۡ لَفِي شَكّٖ مِّنۡهُ مُرِيبٖ
Na hawakutengana wenye kumshirikisha Mwenyezi Mungu katika dini zao wakawa mapote na makundi mbalimbali isipokuwa baada ya ujuzi kuwajia na hoja kuwasimamia. Na hakuna lililowafanya wao wafanye hivyo isipokuwa ni udhalimu na ushindani. Na lao si neno lililotangulia linalotoka kwa Mola wako, ewe Mtume, la kucheleweshwa adhabu mpaka kipindi kilichotajwa. nacho ni Siku ya Kiyama, hukumu ingalitolewa ya kuharakishiwa adhabu wakanushaji miongoni mwao. Na hakika wale waliorithishwa Taurati na Injili, baada ya hawa wenye kutafautiana juu ya haki, wako kwenye shaka yenye kutia kwenye wasiwasi na kutafautiana juu ya Dini na Imani.
Tefsiri na arapskom jeziku:
فَلِذَٰلِكَ فَٱدۡعُۖ وَٱسۡتَقِمۡ كَمَآ أُمِرۡتَۖ وَلَا تَتَّبِعۡ أَهۡوَآءَهُمۡۖ وَقُلۡ ءَامَنتُ بِمَآ أَنزَلَ ٱللَّهُ مِن كِتَٰبٖۖ وَأُمِرۡتُ لِأَعۡدِلَ بَيۡنَكُمُۖ ٱللَّهُ رَبُّنَا وَرَبُّكُمۡۖ لَنَآ أَعۡمَٰلُنَا وَلَكُمۡ أَعۡمَٰلُكُمۡۖ لَا حُجَّةَ بَيۡنَنَا وَبَيۡنَكُمُۖ ٱللَّهُ يَجۡمَعُ بَيۡنَنَاۖ وَإِلَيۡهِ ٱلۡمَصِيرُ
Basi, kwenye dini hiyo iliyolingana sawa ambayo Mwenyezi Mungu Aliwawekea Manabii na Akawausia waifuate, lingania, ewe Mtume, waja wa Mwenyezi Mungu, na uwe na msimamo wa kisawa kama Anavyokuamrisha Mwenyezi Mungu. Na usifuate matamanio ya wale walioifanyia haki shaka na wakapotoka kwa kuwa kando na Dini, na useme, «Nimeviamini Vitabu vyote vilivyoteremshwa kutoka mbinguni kwa Manabiii, Na Mola wangu Ameniamrisha nifanye uadilifu baina yenu katika kuhukumu. Mwenyezi Mungu ni Mola wetu na Mola wenu. Sisi tutapata thawabu ya matendo yetu mema, na nyinyi mtapata malipo ya matendo yenu maovu. Hakuna utesi wala mjadala baina yetu sisi na nyinyi baada ya haki kufafanuka. Mwenyezi Mungu Atatukusanya sisi na nyinyi Siku ya Kiyama Ahukumu baina yetu kwa haki katika yale tuliyotafautiana, na kwake Yeye ndio marejeo na marudio, na huko Amlipe kila mmoja kwa anachostahiki.»
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَٱلَّذِينَ يُحَآجُّونَ فِي ٱللَّهِ مِنۢ بَعۡدِ مَا ٱسۡتُجِيبَ لَهُۥ حُجَّتُهُمۡ دَاحِضَةٌ عِندَ رَبِّهِمۡ وَعَلَيۡهِمۡ غَضَبٞ وَلَهُمۡ عَذَابٞ شَدِيدٌ
Na wale wanaojadili kuhusu Dini ya Mwenyezi Mungu niliyomtumiliza kwayo Muhammad, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie, baada ya watu kuikubali na kusilimu, hoja yao na mjadala wao, mbele ya Mola wao, ni zenye kutenguka na kuondoka. Na watashukiwa na adhabu kutoka kwa Mwenyezi Mungu hapa duniani, na huko Akhera watakuwa na adhabu kali, nayo ni Moto.
Tefsiri na arapskom jeziku:
ٱللَّهُ ٱلَّذِيٓ أَنزَلَ ٱلۡكِتَٰبَ بِٱلۡحَقِّ وَٱلۡمِيزَانَۗ وَمَا يُدۡرِيكَ لَعَلَّ ٱلسَّاعَةَ قَرِيبٞ
Mwenyezi Mungu Ndiye Aliyeteremsha Qur’ani na Vitabu vilivyoteremshwa vinginevyo kwa ukweli. Na Ameteremsha mizani, nayo ni uadilifu, ili Ahukumu baina ya watu kwa usawa. Na ni lipi linalokujulisha na kukufahamisha kuwa huenda wakati ambao Kiyama kitasimama uko karibu?
Tefsiri na arapskom jeziku:
يَسۡتَعۡجِلُ بِهَا ٱلَّذِينَ لَا يُؤۡمِنُونَ بِهَاۖ وَٱلَّذِينَ ءَامَنُواْ مُشۡفِقُونَ مِنۡهَا وَيَعۡلَمُونَ أَنَّهَا ٱلۡحَقُّۗ أَلَآ إِنَّ ٱلَّذِينَ يُمَارُونَ فِي ٱلسَّاعَةِ لَفِي ضَلَٰلِۭ بَعِيدٍ
Wana haraka nako, huko kuja kwa Kiyama, wale wasiokiamini, kwa njia ya shere na mzaha, na wale wanaokiamini wanaogopa kusimama kwake, na hali wao wanajua kuwa ni kweli isiyo na shaka. Basi jua utanabahi kuwa wale wanaojadili kuhusu Kiyama wako kwenye upotevu wa mbali.
Tefsiri na arapskom jeziku:
ٱللَّهُ لَطِيفُۢ بِعِبَادِهِۦ يَرۡزُقُ مَن يَشَآءُۖ وَهُوَ ٱلۡقَوِيُّ ٱلۡعَزِيزُ
Mwenyezi Mungu ni Mpole kwa waja Wake, Anamkunjulia riziki Anayemtaka na Anambania hiyo riziki Anayemtaka, Na Yeye Ndiye Mwenye nguvu ambaye nguvu zote Anazo, Aliye Mshindi katika kuwatesa wenye kumuasi.
Tefsiri na arapskom jeziku:
مَن كَانَ يُرِيدُ حَرۡثَ ٱلۡأٓخِرَةِ نَزِدۡ لَهُۥ فِي حَرۡثِهِۦۖ وَمَن كَانَ يُرِيدُ حَرۡثَ ٱلدُّنۡيَا نُؤۡتِهِۦ مِنۡهَا وَمَا لَهُۥ فِي ٱلۡأٓخِرَةِ مِن نَّصِيبٍ
Yoyote Anayetaka kwa matendo yake malipo mema ya Akhera, Akatekeleza haki za Mwenyezi Mungu na Akatoa katika kulingania Dini, tutamuongezea wema katika matendo yake, tumzidishie thawabu za jema moja mara kumi mpaka kipimo anachokitaka Mwenyezi Mungu cha nyongeza. Na yoyote yule Anayetaka kwa matendo yake ulimwengu peke yake, tutampa tulichomgawia cha huo ulimwengu , na hatakuwa na thawabu zozote huko Akhera.
Tefsiri na arapskom jeziku:
أَمۡ لَهُمۡ شُرَكَٰٓؤُاْ شَرَعُواْ لَهُم مِّنَ ٱلدِّينِ مَا لَمۡ يَأۡذَنۢ بِهِ ٱللَّهُۚ وَلَوۡلَا كَلِمَةُ ٱلۡفَصۡلِ لَقُضِيَ بَيۡنَهُمۡۗ وَإِنَّ ٱلظَّٰلِمِينَ لَهُمۡ عَذَابٌ أَلِيمٞ
Je, kwani hawa wenye kumshirikisha Mwenyezi Mungu wana washirika katika ushirikina wao na upotevu wao ambao waliwazulia katika dini na ushirikina kitu Asichoamuru Mwenyezi Mungu? Na lau si hukumu ya Mwenyezi Mungu makadirio Yake ya kuwapa muhula na kutowaharakishia adhabu duniani, wangalihukumiwa kuharakishiwa adhabu. Na kwa hakika wale wenye kumkanusha Mwenyezi Mungu watakuwa na adhabu yenye uchungu na kuumiza Siku ya Kiyama.
Tefsiri na arapskom jeziku:
تَرَى ٱلظَّٰلِمِينَ مُشۡفِقِينَ مِمَّا كَسَبُواْ وَهُوَ وَاقِعُۢ بِهِمۡۗ وَٱلَّذِينَ ءَامَنُواْ وَعَمِلُواْ ٱلصَّٰلِحَٰتِ فِي رَوۡضَاتِ ٱلۡجَنَّاتِۖ لَهُم مَّا يَشَآءُونَ عِندَ رَبِّهِمۡۚ ذَٰلِكَ هُوَ ٱلۡفَضۡلُ ٱلۡكَبِيرُ
Utawaona, ewe Mtume, makafiri Siku ya Kiyama wako katika hali ya kuogopa mateso ya Mwenyezi Mungu kwa yale matendo mabaya waliyoyatenda duniani, na adhabu itawashukia, na wao wataionja hapana budi. Na wale waliomuamini Mwenyezi Mungu na wakamtii, wataingia kwenye mabustani ya Pepo na majumba yake na starehe za Akhera, na watakuwa na kila kinachotamaniwa na nafsi zao kwa Mola wao. Hayo Aliyowapa Mwenyezi Mungu ya fadhila na utukufu ndiyo nyongeza isiyosifika na isiyofikiwa na akili.
Tefsiri na arapskom jeziku:
ذَٰلِكَ ٱلَّذِي يُبَشِّرُ ٱللَّهُ عِبَادَهُ ٱلَّذِينَ ءَامَنُواْ وَعَمِلُواْ ٱلصَّٰلِحَٰتِۗ قُل لَّآ أَسۡـَٔلُكُمۡ عَلَيۡهِ أَجۡرًا إِلَّا ٱلۡمَوَدَّةَ فِي ٱلۡقُرۡبَىٰۗ وَمَن يَقۡتَرِفۡ حَسَنَةٗ نَّزِدۡ لَهُۥ فِيهَا حُسۡنًاۚ إِنَّ ٱللَّهَ غَفُورٞ شَكُورٌ
Hayo ambayo niliwapa habari kwayo, enyi watu, miongoni mwa starehe na matukufu ya Akhera ndio yale ambayo Mwenyezi Mungu Anawapa bishara kwayo waja Wake wema waliomuamini na kumtii duniani. Sema, ewe Mtume, uwaambie wale wanaofanya shaka kuhusu Kiyama miongoni mwa washirikina wa watu wako, «Siwaombi kwa huu ulinganizi wangu wa haki niliokuja nao mnipe malipo kwenye mali yenu, isipokuwa mnitekelezee haki yangu ya ujamaa kwenu na muunge kizazi kilichoko baina yangu mimi na nyinyi.» Na yoyote mwenye kutenda jema tutamuongezea mara kumi na zaidi. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe kwa wingi dhambi za waja Wake, ni Mwingi wa shukrani kwa mema yao na utiifu wao Kwake.
Tefsiri na arapskom jeziku:
أَمۡ يَقُولُونَ ٱفۡتَرَىٰ عَلَى ٱللَّهِ كَذِبٗاۖ فَإِن يَشَإِ ٱللَّهُ يَخۡتِمۡ عَلَىٰ قَلۡبِكَۗ وَيَمۡحُ ٱللَّهُ ٱلۡبَٰطِلَ وَيُحِقُّ ٱلۡحَقَّ بِكَلِمَٰتِهِۦٓۚ إِنَّهُۥ عَلِيمُۢ بِذَاتِ ٱلصُّدُورِ
Au je, wanasema hawa washirikina, kwamba Muhammad amemzulia Mwenyezi Mungu urongo ndipo akaja na hiki anachokisoma kwa kukizua mwenyewe? Basi Mwenyezi Mungu Ataupiga muhuri moyo wako, ewe Mtume, uwapo utafanya hivyo. Na Mwenyezi Mungu Anaiondoa batili na kuifuta, na Anaithibitisha haki kwa maneno Yake, ambayo hayabadiliki wala hayageuki, na kwa ahadi Yake ya kweli isiyoenda kinyume. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi sana wa yaliyomo ndani ya nyoyo za waja, hakuna chochote kinachofichamana kwake.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَهُوَ ٱلَّذِي يَقۡبَلُ ٱلتَّوۡبَةَ عَنۡ عِبَادِهِۦ وَيَعۡفُواْ عَنِ ٱلسَّيِّـَٔاتِ وَيَعۡلَمُ مَا تَفۡعَلُونَ
Na Mwenyezi Mungu, aliyetakasika na kutukuka, Ndiye Anayekubali toba kutoka kwa waja Wake wanaporudi kwenye kumpwekesha Mwenyezi Mungu na kumtii, Ndiye Anayesamehe makosa na Ndiye Anayejua mnayoyafanya ya kheri na shari, hakuna chochote kinachofichamana Kwake, na Yeye ni Mwenye kuwalipa kwa hayo.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَيَسۡتَجِيبُ ٱلَّذِينَ ءَامَنُواْ وَعَمِلُواْ ٱلصَّٰلِحَٰتِ وَيَزِيدُهُم مِّن فَضۡلِهِۦۚ وَٱلۡكَٰفِرُونَ لَهُمۡ عَذَابٞ شَدِيدٞ
Na wale waliomuamini Mwenyezi Mungu na Mtume Wake, wanamuitika Mola wao kwa kile Alichowaitia na wanajisalimisha Kwake, na Yeye Anawaongezea fadhila Zake kwa kuwaongoza na kuwazidishia malipo na thawabu. Na wale wenye kumkanusha Mwenyezi Mungu na Mtume Wake watapata adhabu kali yenye kuumiza na yenye uchungu Siku ya Kiyama.
Tefsiri na arapskom jeziku:
۞ وَلَوۡ بَسَطَ ٱللَّهُ ٱلرِّزۡقَ لِعِبَادِهِۦ لَبَغَوۡاْ فِي ٱلۡأَرۡضِ وَلَٰكِن يُنَزِّلُ بِقَدَرٖ مَّا يَشَآءُۚ إِنَّهُۥ بِعِبَادِهِۦ خَبِيرُۢ بَصِيرٞ
Na lau Mwenyezi Mungu Angaliwakunjulia riziki waja Wake Akawapa kwa wingi, wangalipita mipaka katika ardhi kwa kiburi na ujeuri na wangalitoka baadhi yao kuwadhulumu wengine. Lakini Mwenyezi Mungu anawateremshia riziki zao kwa kadiri atakayo ya kuwatosha. Hakika Yeye kwa waja Wake ni mtambuzi kwa yale yanayowafaa, Anaiona mipango yao na mabadiliko ya hali zao.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَهُوَ ٱلَّذِي يُنَزِّلُ ٱلۡغَيۡثَ مِنۢ بَعۡدِ مَا قَنَطُواْ وَيَنشُرُ رَحۡمَتَهُۥۚ وَهُوَ ٱلۡوَلِيُّ ٱلۡحَمِيدُ
Na Mwenyezi Mungu Peke Yake Ndiye Anayeteremsha mvua kutoka mbinguni, Akawanyeshea kwayo baada ya kukata tamaa kunyesha kwake, Akaeneza rehema Yake kwa viumbe Vyake, Akawapa mvua ya kuwaenea, na Yeye Ndiye Mtegemewa, Anawasaidia waja Wake kwa hisani Yake na wema Wake, Msifiwa kwa uongozi wake na uendeshaji mambo Wake.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَمِنۡ ءَايَٰتِهِۦ خَلۡقُ ٱلسَّمَٰوَٰتِ وَٱلۡأَرۡضِ وَمَا بَثَّ فِيهِمَا مِن دَآبَّةٖۚ وَهُوَ عَلَىٰ جَمۡعِهِمۡ إِذَا يَشَآءُ قَدِيرٞ
Na miongoni mwa alama za kuonyesha ukubwa Wake, uweza Wake na mamlaka Yake ni uumbaji mbingu na ardhi kwa namna ambayo hakukuwa na mfano uliotangulia na aina mbalimbali za wanyama Alizozieneza humo. Na Yeye, kuwakusanya viumbe baada ya kufa kwao kwa kisimamo cha Kiyama, Anapotaka ni Muweza, hakuna kinachomshinda.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَمَآ أَصَٰبَكُم مِّن مُّصِيبَةٖ فَبِمَا كَسَبَتۡ أَيۡدِيكُمۡ وَيَعۡفُواْ عَن كَثِيرٖ
Na msiba wowote uliowakumba, enyi watu, katika Dini yenu na dunia yenu, ni kwa sababu ya dhambi mlizozitenda na makosa. Na Mola wenu Anawasamehe nyinyi makosa mengi Asiwaadhibu kwa kuyafanya.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَمَآ أَنتُم بِمُعۡجِزِينَ فِي ٱلۡأَرۡضِۖ وَمَا لَكُم مِّن دُونِ ٱللَّهِ مِن وَلِيّٖ وَلَا نَصِيرٖ
Na hamkuwa, enyi watu, ni wenye kushindana na uweza wa Mwenyezi Mungu juu yenu wala kuuhepa. Na hamna nyinyi asiyekuwa Mwenyezi Mungu Mtegemewa wa kusimamia mambo yenu na kuwapa manufaa wala msaidizi wa kuwatetea msipatikane na madhara.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَمِنۡ ءَايَٰتِهِ ٱلۡجَوَارِ فِي ٱلۡبَحۡرِ كَٱلۡأَعۡلَٰمِ
Na miongoni mwa alama Zake zenye kuonyesha uweza Wake mkubwa na mamlaka Yake yenye kushinda ni majahazi makubwa kama majabali yanayotembea baharini.
Tefsiri na arapskom jeziku:
إِن يَشَأۡ يُسۡكِنِ ٱلرِّيحَ فَيَظۡلَلۡنَ رَوَاكِدَ عَلَىٰ ظَهۡرِهِۦٓۚ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَأٓيَٰتٖ لِّكُلِّ صَبَّارٖ شَكُورٍ
Anapotaka Mwenyezi Mungu Anautuliza upepo, na majahazi yakawa ni yenye kutulia juu ya mgongo wa bahari na kutotembea. Hakika katika kutembea majahazi haya na kusimama kwake baharini kwa uweza wa Mwenyezi Mungu pana mawaidha na hoja waziwazi za uweza wa Mwenyezi Mungu, kwa kila mwingi wa uvumilivu juu ya kumtii Mwenyezi Mungu, kujiepusha na vitendo vya kumuasi na kukubali makadirio Yake, mwingi wa shukrani wa neema Zake na mema Yake.
Tefsiri na arapskom jeziku:
أَوۡ يُوبِقۡهُنَّ بِمَا كَسَبُواْ وَيَعۡفُ عَن كَثِيرٖ
Au (Anapotaka) Anayaangamiza hayo majahazi kwa kuyazamisha kwa sababu ya dhambi za wenyewe, na Anasamehe dhambi nyingi Asiwatese wenye kuzifanya.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَيَعۡلَمَ ٱلَّذِينَ يُجَٰدِلُونَ فِيٓ ءَايَٰتِنَا مَا لَهُم مِّن مَّحِيصٖ
Na wajue wale wanaojadili kuhusu aya zetu zenye kutolea dalili upweke wetu kwa njia ya ubatilifu, hawatakuwa na mahali pa kupita wala pa kuhamia kujiepusha na mateso ya Mwenyezi Mungu Atakapowatesa kwa dhambi zao na ukanushaji wao.
Tefsiri na arapskom jeziku:
فَمَآ أُوتِيتُم مِّن شَيۡءٖ فَمَتَٰعُ ٱلۡحَيَوٰةِ ٱلدُّنۡيَاۚ وَمَا عِندَ ٱللَّهِ خَيۡرٞ وَأَبۡقَىٰ لِلَّذِينَ ءَامَنُواْ وَعَلَىٰ رَبِّهِمۡ يَتَوَكَّلُونَ
Na chochote kile mnachopewa, enyi watu, cha mali na watoto na vinginevyo, ni pumbao lenu la uhai wa ulimwenguni, kwa haraka sana litaondoka, na kilichoko kwa Mwenyezi Mungu cha starehe ya Pepo ya daima ni bora zaidi na ni chenye kusalia zaidi kwa wale wenye kumuamini Mwenyezi Mungu na Mitume Wake na wakawa kwa Mola wao wanategemea.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَٱلَّذِينَ يَجۡتَنِبُونَ كَبَٰٓئِرَ ٱلۡإِثۡمِ وَٱلۡفَوَٰحِشَ وَإِذَا مَا غَضِبُواْ هُمۡ يَغۡفِرُونَ
Na wale ambao wanajiepusha na madhambi makubwa yaliyokatazwa na Mwenyezi Mungu, na kila kilichokuwa kichafu na kibaya miongoni mwa maasia, na wanapowakasirikia wale waliowakosea wanaufinika huo ubaya na kuusamehe kwa kuacha kumlipiza mkosa, kwa kutaka malipo mema ya Mwenyezi Mungu Aliyetukuka na msamaha Wake. Na hii ni miongoni mwa tabia njema.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَٱلَّذِينَ ٱسۡتَجَابُواْ لِرَبِّهِمۡ وَأَقَامُواْ ٱلصَّلَوٰةَ وَأَمۡرُهُمۡ شُورَىٰ بَيۡنَهُمۡ وَمِمَّا رَزَقۡنَٰهُمۡ يُنفِقُونَ
Na wale walioitika mwito wa Mola wao wa kumpwekesha Yeye na kumtii, wakasimamisha Swala za faradhi kwa namna zake katika nyakati zake, na wakitaka jambo wanashauriana juu yake , na katika mali tuliyowapa wanatoa sadaka kwenye njia ya Mwenyezi Mungu, na wanatekeleza haki wanazofaradhiwa kuwapatia wanaostahiki kama vile Zaka na matumizi na katika njia nyinginezo za matumizi.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَٱلَّذِينَ إِذَآ أَصَابَهُمُ ٱلۡبَغۡيُ هُمۡ يَنتَصِرُونَ
Na wale ambao yakiwapata maonevu wanawalipiza wale waliowaonea bila kupita kiasi. Na wanaposubiri basi mwisho wa subira yao kuna kheri nyingi.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَجَزَٰٓؤُاْ سَيِّئَةٖ سَيِّئَةٞ مِّثۡلُهَاۖ فَمَنۡ عَفَا وَأَصۡلَحَ فَأَجۡرُهُۥ عَلَى ٱللَّهِۚ إِنَّهُۥ لَا يُحِبُّ ٱلظَّٰلِمِينَ
Na malipo ya ubaya wa mtu mbaya ni kumtesa kwa ubaya mfano wake bila kuzidisha. Na mwenye kumsamehe aliyemfanyia ubaya asimtese, na akatengeneza mapenzi baina yake yeye na yule aliyemsamehe kwa kutaka radhi za Mwenyezi Mungu, basi malipo mema ya kusamehe kwake yako kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu Hawapendi wenye kudhulumu wanaowaanza watu kwa uadui na kuwafanyia ubaya.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَلَمَنِ ٱنتَصَرَ بَعۡدَ ظُلۡمِهِۦ فَأُوْلَٰٓئِكَ مَا عَلَيۡهِم مِّن سَبِيلٍ
Na yoyote aliyemlipiza yule aliyemdhulumu baada ya kudhulumiwa naye, basi hao hawana makosa ya kuadhibiwa kwayo.
Tefsiri na arapskom jeziku:
إِنَّمَا ٱلسَّبِيلُ عَلَى ٱلَّذِينَ يَظۡلِمُونَ ٱلنَّاسَ وَيَبۡغُونَ فِي ٱلۡأَرۡضِ بِغَيۡرِ ٱلۡحَقِّۚ أُوْلَٰٓئِكَ لَهُمۡ عَذَابٌ أَلِيمٞ
Hakika ni kwamba mapatilizo ni ya wale wanaowaonea watu kwa udhalimu na uadui, wakapita mpaka waliowekewa wa vitu walivyohalalishiwa na Mola wao na wakaingia kwenye eneo la vitu visivyoruhusiwa kwao, wakafanya uharibifu katika ardhi pasi na haki, basi hao Siku ya Kiyama watakuwa na adhabu yenye uchungu na kuumiza.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَلَمَن صَبَرَ وَغَفَرَ إِنَّ ذَٰلِكَ لَمِنۡ عَزۡمِ ٱلۡأُمُورِ
Na yoyote mwenye kuvumilia juu ya makero na akalipa, kwa ovu alilofanyiwa, kwa kusamehe, kufuta na kufinika, basi hayo ni miongoni mwa mambo makubwa yenye kushukuriwa na vitendo vyenye kusifiwa ambavyo Mwenyezi Mungu Ameviamrisha na Ameviwekea thawabu nyingi na sifa nzuri.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَمَن يُضۡلِلِ ٱللَّهُ فَمَا لَهُۥ مِن وَلِيّٖ مِّنۢ بَعۡدِهِۦۗ وَتَرَى ٱلظَّٰلِمِينَ لَمَّا رَأَوُاْ ٱلۡعَذَابَ يَقُولُونَ هَلۡ إِلَىٰ مَرَدّٖ مِّن سَبِيلٖ
Na yule ambaye Mwenyezi Mungu Anampoteza na kumweka kando na uongofu kwa sababu ya udhalimu wake, hatakuwa na mtu wa kumsaidia na kumuelekeza njia ya uongofu. Na utawaona, ewe Mtume, wenye kumkanusha Mwenyezi Mungu Siku ya Kiyama, watakapo kuiona adhabu, wakisema, kumwambia Mola wao, «Je, tuna njia yoyote ya kurejea duniani ili tufanye matendo ya utiifu kwako?» Na ombi hilo halitakubaliwa kwao.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَتَرَىٰهُمۡ يُعۡرَضُونَ عَلَيۡهَا خَٰشِعِينَ مِنَ ٱلذُّلِّ يَنظُرُونَ مِن طَرۡفٍ خَفِيّٖۗ وَقَالَ ٱلَّذِينَ ءَامَنُوٓاْ إِنَّ ٱلۡخَٰسِرِينَ ٱلَّذِينَ خَسِرُوٓاْ أَنفُسَهُمۡ وَأَهۡلِيهِمۡ يَوۡمَ ٱلۡقِيَٰمَةِۗ أَلَآ إِنَّ ٱلظَّٰلِمِينَ فِي عَذَابٖ مُّقِيمٖ
Na utawaona, ewe Mtume, hawa madhalimu wakiorodheshwa Motoni wakiwa wadhalilifu na wanyonge, wanakutazama kwa jicho la unyonge lililo dhaifu kwa hofu waliokuwa nayo na utwevu. Na watasema waliomuamini Mwenyezi Mungu na Mtume Wake Peponi, watakapoyaona yaliyowashukia makafiri ya hasara, «Hakika wenye hasara kikweli ni wale waliopata hasara ya nafsi zao na watu wao Siku ya Kiyama kwa kuingia Motoni.» Jua utanabahi kuwa madhalimu, siku ya Kiyama, watakuwa kwenye adhabu ya daima isiyokatika wala kuondoka.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَمَا كَانَ لَهُم مِّنۡ أَوۡلِيَآءَ يَنصُرُونَهُم مِّن دُونِ ٱللَّهِۗ وَمَن يُضۡلِلِ ٱللَّهُ فَمَا لَهُۥ مِن سَبِيلٍ
Na hawa wenye kukanusha, Atakapowaadhibu Mwenyezi Mungu Siku ya Kiyama, hawatakuwa na wasaidizi na waokozi wenye kuwanusuru kutokana na adhabu ya Mwenyezi Mungu. Na yoyote yule ambaye Mwenyezi Mungu Amempoteza kwa sababu ya ukanushaji wake na udhalimu, hatakuwa na njia yenye kumfikisha kwenye haki hapa duniani, na kwenye Pepo kesho Akhera, kwa kuwa yeye atakuwa amezibiwa njia za kuokoka, kwani kuongoza na kupoteza viko mkononi mwa Mwenyezi Mungu, kutakasika na kutukuka ni Kwake, na haviko kwa mwingine.
Tefsiri na arapskom jeziku:
ٱسۡتَجِيبُواْ لِرَبِّكُم مِّن قَبۡلِ أَن يَأۡتِيَ يَوۡمٞ لَّا مَرَدَّ لَهُۥ مِنَ ٱللَّهِۚ مَا لَكُم مِّن مَّلۡجَإٖ يَوۡمَئِذٖ وَمَا لَكُم مِّن نَّكِيرٖ
Itikieni mwito wa Mola wenu, enyi wenye kukanusha, kwa kuamini na kutii kabla haijaja Siku ya Kiyama ambayo haimkiniki kuirudisha. Siku hiyo hamtakuwa na mahali pa kukimbilia penye kuwaokoa na adhabu wala mahali pa kuwasitiri mkawa hamtambulikani hapo. Katika aya hii pana dalili ya ubaya wa kuchelewesha, na pana maamrisho ya kuharakisha kufanya kila tendo zuri linalomtokea mja, kwani kuchelewesha kuna athari mbaya na vizuizi.
Tefsiri na arapskom jeziku:
فَإِنۡ أَعۡرَضُواْ فَمَآ أَرۡسَلۡنَٰكَ عَلَيۡهِمۡ حَفِيظًاۖ إِنۡ عَلَيۡكَ إِلَّا ٱلۡبَلَٰغُۗ وَإِنَّآ إِذَآ أَذَقۡنَا ٱلۡإِنسَٰنَ مِنَّا رَحۡمَةٗ فَرِحَ بِهَاۖ وَإِن تُصِبۡهُمۡ سَيِّئَةُۢ بِمَا قَدَّمَتۡ أَيۡدِيهِمۡ فَإِنَّ ٱلۡإِنسَٰنَ كَفُورٞ
Watakapokataa hawa washirikina, ewe Mtume, kumuamini Mwenyezi Mungu, basi hatukukutumiliza kuwa ni mtunzi wa matendo yao mapaka ukawa ni mwenye kuwahesabu kwa hayo. Lazima yako haikuwa isipokuwa ni kufikisha ujumbe. Na sisi tunapompa binadamu rehema kutoka kwetu rehema ya utajiri, ukunjufu wa mali na mengineyo, hufurahika na akapendezwa, na unapowakumba msiba wa umasikini, ugonjwa na mengineyo kwa sababu ya kile kilichotangulizwa na mikono yao cha kufanya matendo ya kumuasi Mwenyezi Mungu, hapo binadamu huwa ni mwenye kukataa sana, huwa akihesabu misiba na akisahau neema.
Tefsiri na arapskom jeziku:
لِّلَّهِ مُلۡكُ ٱلسَّمَٰوَٰتِ وَٱلۡأَرۡضِۚ يَخۡلُقُ مَا يَشَآءُۚ يَهَبُ لِمَن يَشَآءُ إِنَٰثٗا وَيَهَبُ لِمَن يَشَآءُ ٱلذُّكُورَ
Ni ya Mwenyezi Mungu mamlaka ya mbingu na ardhi na vilivyomo ndani yake. Anaumba viumbe anavyovitaka. Anamtunuku Anayemtaka miongoni mwa waja Wake wanawake bila kuwa na wanaume pamoja nao, na Anamtunuku Anayemtaka wanaume bila kuwa na wanawake pamoja nao.
Tefsiri na arapskom jeziku:
أَوۡ يُزَوِّجُهُمۡ ذُكۡرَانٗا وَإِنَٰثٗاۖ وَيَجۡعَلُ مَن يَشَآءُ عَقِيمًاۚ إِنَّهُۥ عَلِيمٞ قَدِيرٞ
Na Anampa, Anayetakasika na kutukuka, Anayemtaka miongoni mwa watu wanaume na wanawake. Na Anamfanya Anayemtaka kuwa tasa asiyezaa. Hakika Yeye ni Mjuzi sana wa Anachoumba, ni Muweza sana kuumba Anachotaka, hakuna chochote kinachomshinda Akitaka kukiumba.
Tefsiri na arapskom jeziku:
۞ وَمَا كَانَ لِبَشَرٍ أَن يُكَلِّمَهُ ٱللَّهُ إِلَّا وَحۡيًا أَوۡ مِن وَرَآيِٕ حِجَابٍ أَوۡ يُرۡسِلَ رَسُولٗا فَيُوحِيَ بِإِذۡنِهِۦ مَا يَشَآءُۚ إِنَّهُۥ عَلِيٌّ حَكِيمٞ
Na haipasi kwa kiumbe yoyote, kati ya binadamu, Mwenyezi Mungu Aseme naye isipokuwa kwa njia ya wahyi ambao Mwenyezi Mungu Anamtumia au Aseme naye nyuma ya pazia, kama vile Alivyosema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika, na Mūsā, amani imshukie, Au Atume mjumbe, kama Anavoyomtuma Jibrili, amani imshukie, kwa yule anayetumwa kwake ampelekee wahyi wa kile Mwenyezi Mungu Anataka apelekewe, kwa idhini ya Mola wake, na sio kwa mapendeleo yake. Hakika Yake Yeye, Aliyetukuka, Yuko juu kwa dhati Yake, majina Yake, sifa Zake na vitendo Vyake. Amekilazimisha kila kitu, na viumbe vyote vimemdhalilikia, ni Mwingi wa hekima katika uedeshaji Wake mambo ya viumbe Vyake. Katika aya hii pana kuthibitisha sifa ya kusema kwa Mwenyezi Mungu Aliyetukuka kwa namna inayonasibiana na haiba Yake na ukubwa wa mamlaka Yake.
Tefsiri na arapskom jeziku:
وَكَذَٰلِكَ أَوۡحَيۡنَآ إِلَيۡكَ رُوحٗا مِّنۡ أَمۡرِنَاۚ مَا كُنتَ تَدۡرِي مَا ٱلۡكِتَٰبُ وَلَا ٱلۡإِيمَٰنُ وَلَٰكِن جَعَلۡنَٰهُ نُورٗا نَّهۡدِي بِهِۦ مَن نَّشَآءُ مِنۡ عِبَادِنَاۚ وَإِنَّكَ لَتَهۡدِيٓ إِلَىٰ صِرَٰطٖ مُّسۡتَقِيمٖ
Na kama vile tulivyowapelekea wahyi Manabii kabla yako wewe, ewe Nabii, tulikuletea wewe wahyi wa Qur’ani itokayo kwetu, hukuwa unajua kabla yake ni vitabu vipi vilivyotangulia wala nini Imani wala zipi Sheria zinazotokana na Mwenyezi Mungu? Lakini tumeifanya Qur’ani ni mwangaza kwa watu ambao kwa huo tunawaongoza waja wetu tunaowataka kwenye njia iliyolingana sawa. Na hakika wewe, ewe Mtume, unamuelekeza na kumuongoza kwa amri ya Mwenyezi Mungu kwenye njia iliyolingana sawa, nayo ni Uislamu,
Tefsiri na arapskom jeziku:
صِرَٰطِ ٱللَّهِ ٱلَّذِي لَهُۥ مَا فِي ٱلسَّمَٰوَٰتِ وَمَا فِي ٱلۡأَرۡضِۗ أَلَآ إِلَى ٱللَّهِ تَصِيرُ ٱلۡأُمُورُ
njia ya Mwenyezi Mungu Aliye na mamlaka ya vyote vilivyoko mbinguni na vilivyoko ardhini, hana mshirika katika hayo. Jua utanabahi kwamba kwa mwenyezi Mungu , enyi watu, yatarudi mambo yote yenu ya kheri na shari, na huko Amlipe kila mtu kwa matendo yake, yakiwa mema alipwe wema na yakiwa mabaya alipwe ubaya.
Tefsiri na arapskom jeziku:
 
Prijevod značenja Sura: Sura eš-Šura
Indeks sura Broj stranice
 
Prijevod značenja časnog Kur'ana - الترجمة السواحلية - عبد الله محمد وناصر خميس - Sadržaj prijevodā

ترجمة معاني القرآن الكريم إلى اللغة السواحلية، ترجمها الدكتور عبد الله محمد أبو بكر والشيخ ناصر خميس.

Zatvaranje